Na JENNIFER ULLEMBIO-DAR ES SALAAM
MSANII wa Bongo Fleva, Vanesa Mdee ‘V Money’, amesema kuwa bado hajafikia hata robo ya malengo aliyojiwekea kuyafanya kupitia fani ya muziki.
Akizungumza na MTANZANIA, V money alisema anakabiliwa na kibarua kizito kuhakikisha anasonga mbele na kupiga hatua zaidi ya sasa.
Alisema wasanii wengi wamekuwa wakimpa pongezi na kumsifia kwa hatua aliyofikia, anashukuru ila bado upande wake hakuna chochote anachoweza kujisifia.
“Mimi kama mimi bado naona sijafikia hata robo ya malengo ninayotarajia kuyapata kupitia muziki, ila nashukuru wale wanaonipongeza kila kukicha,” alisema V Money.
Mwanadada huyo anayetamba na wimbo wake wa Kisela, alieleza kuwa ataendelea kupambana zaidi na zaidi ili kuutangaza muziki wa Tanzania na kutangaza kipaji chake.