29.2 C
Dar es Salaam
Friday, May 3, 2024

Contact us: [email protected]

UTATA WA UMRI WAAHIRISHA KESI YA BILIONEA MSUYA

 

Na Upendo Mosha-Moshi


MAHAKAMA Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, imelazimika kuahirisha kwa muda kesi ya mauaji ya mfanyabiashara wa madini, Erasto Msuya,  aliyeuawa kwa kupigwa risasi, kutokana na mkanganyiko wa umri wa mjumbe wa Baraza la Mahakama.

Kuahirishwa kwa kesi hiyo kunatokana na kuibuka hoja ya kupita umri wa sheria wa mzee wa baraza, Mery John ambaye anadaiwa kuwa na umri zaidi ya miaka 60 huku sheria ikitaka umri kati ya miaka 21 hadi 60.

Hoja hiyo ya sheria iliibuliwa mahakamani hapo jana na Wakili Mwandamizi wa upande wa Jamhuri, Abdallah Chavula, akiwawakilisha mawakili wa Serikali, Kasim Nasri, Omari Kibwana na Lucy Kyusa.

“Mheshimiwa Jaji katika kupitia kumbukumbu zetu za mwenendo wa shauri hili assessor  (mzee wa baraza) Mery John, tarehe tano mwezi wa 10 mwaka 2015 alikuwa na umri wa miaka 59 na kwa mujibu wa kifungu cha 266 (1) cha sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai kinaweka sharti la lazima  la mtu kuwa Assessor.

“Leo ni tarehe 18  mwezi wa 10 mwaka 2017 umri wake ni zaidi ya miaka 60 hivyo ni wazi umri wake umevuka hitaji la sheria,”alisema.

Mkanganyiko huo wa umri ulitokana na kupungua akidi ya wajumbe wa baraza kutoka watatu hadi kufikia wawili, baada ya mjumbe mmoja Zacharia Nato kufariki dunia na kubaki wawili ambao ni Mery John na Herry Msangi.

Wakati  mkanganyiko  huo ukijitokeza, Wakili Chavula aliieleza Mahakama kuwa ikiwa mjumbe mmoja kati ya wawili waliobaki ataondolewa kesi hiyo italazimika kuanza upya.

“Washitakiwa wamekaa muda mtrefu tangu mwaka 2013 na hawajui hatima ya shauri lao na upande wa mashitka utalazimika kuanza kutafuta mashahidi upya hivyo tunaomba mahakama kutokana na athari hizo itumie busara katika umri wa mjumbe wa mahakama.

Katika kesi hiyo upande wa utetezi wa unawakilishwa na Wakili Majura Magafu, uliunga mkono hoja hiyo.

Alisema kuwa baada ya kushauriana na wateja wao wote kwa pamoja walikubaliana shauri hilo liendelee kusikilizwa.

“Mheshimiwa Jaji sisi wote pamoja na wateja wetu tumekaa tunaona  ni vema shauri hili liendelee na mahakama itoe muda kwa mjumbe wa makahama kuendelea hadi mwisho wa kesi hii na umri usiwe sababu kwa sababu  sheria inaruhusu mahakama kujiwekea utaratibu kuhusiana na mashauri ya jinai,” alisema.

Jaji anayesikiliza kesi hiyo, Salma Maghimbi, alikubalina na hoja zilizotolewa na upande wa Jamhuri na ule wa utetezi na alikubali kuendelea kuendelea na mjumbe huyo hadi hapo kesi hiyo itakapomalizika.

Hata hivyo baada ya mahakama kutoa uamuzi, shahidi wa tisa, Inspekta Samuel Maimu aliendelea kutoa ushahidi wake  akidai kuwa siku ya tukio alifika eneo husika na kukusanya maganda 22 ya risasi alizopigwa marehemu Ersto msuya.

Msuya aliuawa Agosti 7 mwaka 2013 saa 6:30 mchana, kando mwa Barabara Kuu ya Arusha/Moshi, karibu na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA).

Kesi hiyo namba 12 ya mwaka 2014 inawakabili washtakiwa saba  ambao ni Sharifu Mohamed, mfanyabishara Shahibu Said na  Mussa Mangu.

Wengine ni Jalila Saidi, Sadiki Jabiri, Karim Kihundwa  na Ally Mussa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles