23.3 C
Dar es Salaam
Wednesday, May 8, 2024

Contact us: [email protected]

UNAJUA KILICHOPO KWENYE NDOA?

NINAANDIKA mada hii nikiwa na uhakika kwamba vijana wengi wa sasa wanatamani kuingia kwenye ndoa na wapenzi wao wakiwa na mitazamo mbalimbali; mingi mizuri.

Nasema hivyo nikimaanisha kuwa, wanaamini wakiwa kwenye ndoa watatimiza ndoto zao za muda mrefu. Hupiga picha kuhusu idadi ya watoto watakaozaa, namna watakavyowasomesha na jinsi ambavyo familia yao itakuwa yenye furaha.

Kifupi wanafikiria zaidi kuhusu mambo ambayo yatawafurahisha. Kamwe hawapati muda wa kufikiria namna ya kukabiliana na changamoto mbalimbali za maisha watakazokutana nazo.

Hawaelewi kwamba kuna siku wanaweza kukaa wiki nzima ndani bila kuzungumza. Je, ni kweli kwamba ndoa ni furaha tu? Hakuna huzuni? Hakuna ugomvi?

Rafiki zangu, hata viongozi wa dini, wanapofungisha ndoa, husisitiza kuhusu kuvumiliana, kutunzana na kupendana kwa dhati hata katika kipindi cha shida na raha.

Kwa bahati mbaya, baadhi ya rafiki zetu wanapokea tofauti maneno haya, wanaamini kwa kuambiwa hivyo, humaanisha kwamba kupendana labda hata kama fedha ya kula itakosekana nyumbani, mwenzake akiumwa n.k.

Huo ni mtazamo tasa. Katika mada hii nitakufumbua, ujue nini zaidi utakutana nacho ukiwa ndani ya ndoa. Twende darasani.

 

FIKRA ZA WENGI

Kama nilivyoeleza hapo juu, fikra za wengi ni tofauti. Asilimia kubwa wanafikiria zaidi kuhusu maisha mazuri yasiyo na mikwaruzano. Wanawaza kufurahia ndoa na kudhani hakuna changamoto nyingine.

Wapo wanaofikiria hata suala la tendo la ndoa. Kwamba watakuwa huru kukutana kila siku kadiri watakavyoweza kwa kuwa wapo pamoja ndani. Hii ni mitazamo mibaya sana katika ndoa.

Ni kweli unaweza kufanya tendo la ndoa na mwenzako mara nyingi uwezavyo, lakini nani amekudanganya kwamba kila siku utaendelea kumuona kama umuonavyo leo?

Amini usiamini, zipo ndoa nyingi zinazolalamikia suala la tendo la ndoa. Kuna ambao wanadai hawatoshelezwi huku wengine wakilalama kuwa wenzi wao hawataki kabisa kutoa unyumba.

Unajua kwa nini? Ama ana mtu mwingine pembeni au amechoshwa na mapenzi ya aina moja kila siku.

 

(i) Wanaume

Hawa fikra zao huwa kwenye suala la usafi, wanaamini wakiwa kwenye ndoa nyumba itakuwa safi, nguo zitafuliwa, kupikiwa na mambo mengine ya kifamilia.

Akili zao zinakomea hapo tu, hawawazi kuhusu migogoro na namna ya kutatua. Wanaota kuwa na maisha mazuri, kuwa na watoto na kujijengea heshima kwa jamii. Hilo tu, basi!

 

(ii) Wanawake

Baadhi ya hawa ninaowazungumzia hufikiria kuhusu kuvaa vizuri, kutolewa out, kupata watoto na mengineyo. Kamwe hawana muda wa kufikiria juu ya matatizo ambayo yanaweza kutokea katika maisha ya ndoa.

Hili ni tatizo. Rafiki zangu, maisha ya ndoa hayana furaha siku zote. Kuna wakati dhoruba hutokea na kusababisha mifarakano hivyo kuhitajika umakini wa hali ya juu katika kumaliza tatizo. Si kila siku kuna amani.

 

TATIZO LIPO WAPI?

Kwa wale ambao wana mitazamo ambayo nimeeleza hapo juu, huwa hawana muda kwanza wa kuwachunguza wapenzi wao, lakini pia wao wenyewe kuonesha tabia zao halisi ili wenzi wao waweze kuwasoma kama wataweza kuendana nao.

Rafiki zangu, kwa ujumla hatutakiwi kufikiria mazuri pekee kwenye ndoa, kuna mengi ya kuvumiliana.

 

ISHI MAISHA YAKO HALISI

Huwezi kumjua mwenzako kama atakuwa anaishi kisanii na wewe. Sikiliza… kwa wiki mnakutana mara mbili tu, tena mnakaa kwa muda usiozidi masaa mawili, si rahisi sana kuweza kujuana tabia zenu halisi.

Pamoja na hayo, wataalamu wa mambo ya mapenzi wanashauri ili mwenzi aweze kuwa wazi zaidi kwa mwenzake ni vyema yeye akaanza kuwa wazi na kuishi maisha yake halisi kwa uwazi.

Usijilazimishe kupenda kitu ambacho hukipendi. Kama kuna jambo ambalo analifanya na linakuboa, mwambie ajue ukweli.

Kwanza, uwazi wako kwake utamfanya naye awe wazi kwako. Hatakuwa na sababu ya kuigiza maisha wakati wewe unaishi maisha yako halisi.

Kila mmoja akimjua mwenzake, ndoa haiwezi kuwa na matatizo, maana kila mtu atakuwa anajua anaishi na mtu wa aina gani.

Inawezekana kabisa, mmoja wenu akaona tabia za mwenzake zimemshinda. Kama ni kweli na umegundua kwamba kuingia kwenye ndoa ni sawa na utumwa, fanya maamuzi!

Wiki ijayo tutaendelea, USIKOSE!

 

Jiandae kupata kitabu changu kipya cha SIRI ZA NDOA YENYE FURAHA kitakachokuwa mitaani hivi karibuni.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
587,000SubscribersSubscribe

Latest Articles