25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Serikali yataja sababu tatu kuadimika sukari

RAMADHAN HASSAN -DODOMA

 SERIKALI imetaja sababu tatu ambazo zimesababisha kuadimika kwa sukari nchini, huku ikitoa msimamo wake kuhusu bihaa hiyo muhimu.

Waziri wa Kilimo, Japhet Hasunga alisema bungeni jana kuwa sababu hizo ni ugonjwa wa corona, baadhi ya wanunuzi kuficha sukari, meli nyingi zimekuwa zikifaulisha mizigo kwenye meli nyingine hivyo kusababisha kuchelewa kufika kwa wakati nchini.

Hasunga alisema hayo jana bungeni, alipokuwa akiwasilisha bajeti ya wizara yake ya mwaka wa fedha 2020/21 jijini Dodoma, ambapo aliomba Bunge liwaidhibishie zaidi ya Sh bilioni 229.8.

Kutokana na hali hiyo, alisema kuwa ili kukabiliana na na changamoto ya ukosefu wa sukari, Serikali ilitoa vibali vya kuagiza sukari tani 40,000 kutoka nje ya nchi.

Alisema kikao cha pamoja na wawakilishi wa uzalishaji, Serikali na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na Bodi ya Sukari chini ya usimamizi wa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, walikubaliana kutokupandishwa kwa bei za sukari.

“Hata hivyo kumejitokeza kuchelewa kuingia nchini kutokana na Covid-19 , baadhi ya wanunuzi kuficha sukari imekuwa ni tatizo. Wizara kupitia Bodi ya Sukari ilifanya uchunguzi wa kina na kwa kutumia sheria ya tasnia ya sukari ilichukua hatua ya kutangaza bei elekezi ya jumla na rejareja katika mikoa yote ya Tanzania Bara kwa lengo la kukabiliana na wafanyabiashara wasio waaminifu.

“Sasa hivi ni kweli katika maeneo mbalimbali kuna upungufu wa Sukari, ni kutokana na meli nyingi zimekuwa zikifaulisha kwenye meli nyingine hivyo haiji kadri unavyotakiwa,” alisema Hasunga.

TANI ZILIZOWASILI MPAKA SASA

Hasunga alisema mpaka kufikia Mei 10 mwaka huu tani zilizokuwa zimewasili nchini ni 4,000 huku tani 21,000 zikitarajiwa kuwasili mwezi huu.

“Tani 500 zimetoka Afrika ya Kusini zimeshafika hivyo hatutegemei kuwa na upungufu wa sukari, mahitaji ni tani 35,000 kwa mwezi hivyo ilivyoingizwa ni tani 40,000 na waliamini itatosha maana viwanda ilikuwa vianze uzalishaji Mei mwishoni.

“Lakini kutokana na mvua kuendelea kunyesha na kiwanda kimoja tu kimeonyesha dalili ya kuanza uzalishaji mwisho wa mwezi,” alisema Hasunga.

SUKARI IPO

Aidha Waziri huyo wa Kilimo, aliwatoa hofu Watanzania kwa kudai kwamba Sukari ipo ya kutosha.

“Niwahakikishie Watanzania kuwa Sukari iliyoingia na hatua zilizochukuliwa kwani sukari inatosha kabisa na hatuhitaji kuwa na upungufu. Niwaombe wenzangu wanaohusika wahakikishe sukari iliyofika wanaiotoa na kusimamia usambazaji katika mikoa yote nchini.

“Tumekokotoa bei ya sukari inayotoka nje mpaka inafika Dar es Dalaam ni Dola 350 (zaidi ya Sh 800,000), mpaka nchi za mbali kama Brazil ni dola 500 (zaidi ya Sh milioni moja) , tukikikokotoa kwa bei ya Tanzania Sukari haitakiwi kuzidi bei tulizotangaza,” alisema.

Waziri Hasunga alisema walikaa kikao na Waziri Mkuu na waagizaji wa Sukari nchini ambapo wagizaji hao walikubali kutopandisha bei ya sukari. 

“Na tumekaa jana (juzi) chini ya Waziri Mkuu na waagizaji wa Sukari wametuahidi kabisa bei haitakiwi kupanda hivyo katika sukari inayokuja itauzwa kwa bei ile tuliyoizoea,” alisema.

CHAKULA KUUZWA NJE KWA MTANDAO

Akijibu hoja za wabunge wakati wa kuhitimisha bajeti, Hasunga alisema Serikali itatumia mfumo wa mtandao kuuza mazao yake nje ya nchi kutokana na janga la corona.

Alisema kutokana na changamoto ya corona Serikali imejipanga kutumia kuuza mazo kwa kutumia mtandao.

“Kutokana na janga la corona kwa sasa kutakuwa na changamoto lakini tumejipanga kutumia kuuza kwa kutumia mtandao,”alisema.

Pia tumejipanga kutumia balozi za nje kwa kuongea na wanunuzi kwa wafanyabiashara wanaohitaji bidhaa.

Alisema ili kilimo kiweze kufanya vizuri lazima wizara ijikite kwenye pembejeo pamoja na utafiti.

“Kama tutaweza kufanya vizuri katika utafiti kilimo cha kisasa wakatumia mbolea na mbegu nzuri tutakuwa na chakula cha kutosha na tutajenga uchumi imara. Katika mwaka ambao matumizi ya mbolea yamekuwa ni makubwa ni mwaka huu tulipanga kutumia tani 586,500 hadi leo zimetumika tani 633,000 zaidi ya kile. 

“Mheshimiwa Spika kwa timu hii tumelisimamia mwaka huu tumelisimamia mwaka huu hatujapata mbolea feki na zimefika kila mahali.

“Tunachokisema kila Mtanzania mwenye uwezo wa kulima sasa wakati ndio huu, mbegu zitakuja kwa wakati mbolea zitakuja kwa wakati viwatilifu vitakuja kwa wakati kazi ipo katika kilimo.

“Nchi za jirani hazitakuwa na chakula cha kutosha lakini nchi zingine hazina chakula cha kutosha, ninachowaomba Watanzania katika hichi chakula watakachokuwa nacho wasikimbilie kukiuza,”alisema. 

Naye, Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Omari Mgumba alisema Serikali imechukua hatua katika kukabiliana na wanaouza sukari bei ya juu.

“Tumeanza kuchukua hatua na wale wezi wa sukari hatutaingilia biashara lakini tutamlinda mlaji,Huu uhuni unaofanyika hatuwezi kuukubali mtu akikuuzia shilingi 4000 au 5000 dai risiti au toa taarifa kwa wahusika,”alisema. 

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe alisema wizara itahakikisha mkulima ateswi na zao lake mwenyewe kwa Serikali kuhakikisha ananufaika. 

“Ni vizuri wakulima wakafahamu fedha zilizopo nje ya bajeti ni zaidi ya shilingi trilioni 3 ni lazima tukubali kuna upungufu wa fedha za bajeti na ni lazima fedha za kilimo ziende kumsaidia mkulima mambo ya semina hapana,”alisema.

Wabunge 

Mbunge wa Nanyamba, Abdallah Chikota(CCM) aliiomba Wizara ya Kilimo kuunda tume ya wataalamu kwa ajili ya kushughulikia ushirika kwani kwa sasa imekuwa sio kimbilio la wakulima. 

“Ushirika nilitegemea uwe kimbilio la wakulima lakini tatizo ni nini ushirika sio kimbilio la wakulima. Ningependekeza Waziri wa Kilimo unda timu ya wataalamu wauchunguze ushirika ili waje na mapendekzo ili kama tatizo ni sheria ije bungeni turekebishe ili tujenge ushirika unaojibu kero za walima,”alisema.

Pia aliiomba wizara hiyo kushuhulikia changamoto ya vifungashio katika korosho kwani ubora wake umekuwa ukipungua.

“Naishauri Serikali ni suala la vifungashio naiomba wizara ilisimamie jambo hili kwani ubora wa korosho zinaharibika. Suala la upatikanaji wa vifungashio naomba hata vyama vya suhirika vipewe nafasi,”alisema.

Mbunge huyo alishauri pembejeo zipatikanae kwa wakati ili zao la Korosho liwe na ubora. 

“Pembejeo ipatikanae kwa wakati na iwe na ubora ili zisiathiri zao letu la Korosho kwani zinaporomosha ubora wa Korosho.

 Mbunge wa Viti Maalum, Fatma Toufiq (CCM) alisema miradi yenye changamoto inatakiwa kuundiwe tume ili iweze kuwa na tija

“Mbegu za zabibu zinatakiwa kufanyiwa utafiti ili ziweze kuwa zenye tija,”alisema.

Mbunge wa Ulanga, Goodluck Mlinga (CCM) aliiomba Wizara ya Kilimo kutoa ufafanuzi kuhusiana na stakabadhi ghalani kwani imekuwa ikiwachanganya wakulima wa ufuta katika jimbo lake.

Mbunge wa Muleba Kaskazini, Charles Mwijage (CCM) alisema mvua zinazoendelea kunyesha zinatakiwa kuwa fursa katika kilimo cha umwagiliaji. 

“Hizi mvua zilizokuja tuzione ni fursa madimbwi ya maji muyatumie ili itusaidie tatizo la chakula.Nawaomba Wizara ya Kilimo msiwe na haraka ya kuuza chakula nje.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles