22.5 C
Dar es Salaam
Saturday, May 11, 2024

Contact us: [email protected]

RC apiga marufuku watoto minada ya mifugo

MWANDISHI WETU – SHINYANGA

MKUU wa Mkoa wa Shinyanga, Zainabu Tellack amewataka wazazi na walezi mkoani Shinyanga,  kutowaruhusu watoto wadogo kwenda katika mikusanyiko hususani minada ya mazao na mifugo kama hatua muhimu ya kuwakinga na maambukizi ya ugonjwa wa corona.

Mkuu wa Mkoa ameyasema hayo, mwishoni mwa wiki wakati alipotembelea mnada wa mifugo wa Muhunze ulioko katika Makao Makuu ya Wilaya ya Kishapu Mkoani Shinyanga kwa lengo la kujionea utekelezaji wa agizo la serikali linalowataka wananchi kuchukua tahadhari ya kujikinga na  ugonjwa wa corona ikiwemo kuweka maji na sabuni katika maeneo yanayokutanisha watu wengi pamoja na kukaa  umbali wa mita moja.

Tellack alionya kuwa huu si wakati wazazi kutembea na watoto wao kutokana na uwepo wa mlipuko wa ugonjwa wa corona na kuwataka kusubiri mpaka wakati ugonjwa huu utakapokuwa umedhibitiwa kwani uwezo wa watoto kujikinga ni mdogo sana.

Pamoja na agizo hilo la Mkuu wa Mkoa kwa wakazi na wafanyabiashara katika minada ya mifugo pia hakuridhishwa na hatua za zuinazochukuliwa na uongozi wa mnada huo za kuhakikisha wale wote wanaoingia mnadani hapo wanasafisha mikono yao baada ya kujionea mnada huo ukiwa na njia zaidi ya moja ya kuingia mnadani hapo na kutoa nafasi kwa baadhi ya watu kujipenyeza ndani ya eneo hilo bila kuchukua tahadhari ya kujikinga na Corona.

Hata hivyo aliwataka wafanyabiashara mnadani hapo kuhakikisha wanajikinga na maambukizi hayo kwa kila mmoja kunawa mikono yake kila mara na kuhakikisha wanakuwa na vitakasa mikono (sanitizers) kwa vile wanao uwezo wa kuvinunua kama hatua muhimu ya kujikinga na hatari ya maambukizi hayo.

“Nunueni vitakasa mikono kwa ajili ya usalama wenu kwa sababu hamuwezi kukosa fedha ya kununua ya kiasi cha shilingo elfu nne na miatano na hata kama ni shilingi elfu kumi kwa ajili ya kujikinga na kuwakinga wengine,’’ alisema Tellack

Agizo kama hilo pia lilitolewa na Mkuu wa Mkoa kwa wafanyabiashara ndogo wanaofika eneo la mnada kwa lengo la kujipatia kipato tofauti na mifugo inayouzwa mnadani kuhakikisha wanakuwa na maji na sabuni vinginevyo watozwe faini kwa kushindwa kutekeleza agizo hilo muhimu la Serikali.

Pamoja na kutembelea mnada huo mkuu huyo wa mkoa pia alitembelea Kituo cha Afya cha Wilaya ya Kishapu kilichoandaliwa kama sehemu maalumu ya kupeleka wagonjwa wa corona endapo watabainika Wilayani humo kama hatua muhimu ya kujionea ni namnagani Wilaya ya Kishapu imejipanga kukabiliana na ugonjwa huo.

Akiwa katika kituo hicho cha Afya Mkuu wa Mkoa alijionea vifaa vnitakovyotumiwa na waudumu wa Afya kujikinga na kuwahudumia wagonjwa na kuwataka wahudumu hao kuwa tayari kwa lengo la kukabiliana na kuhudumia wagonjwa hao kwa tahadhari kubwa.

Mnada huo unaowakutanisha wafanyabiashara wa mifugo kutoka sehemu mbalimbali za mkoa wa Shinyanga na mikoa jilani ufanyika kila Siku ya Alhamisi na kuvuta wafanyabiashara wa aina nyingine nje na ndani ya mnada huo ambao pia wametakiwa kuchukua tahadhari kwa kuweka vitakasa mikono katika maeneo yao ya biashara.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
587,000SubscribersSubscribe

Latest Articles