25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Rais Mwinyi: Sitasita kumchukulia hatua Mtendaji atakayebainika kufanya udhalilishaji

Na Mwandishi Wetu, Zanzibar

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Husein Ali Mwinyi amesema kuwa hatosita kumchukulia hatua mtendaji yoyote aliyemteua ambaye atabainika kujihusisha ni vitendo vya udhalilishaji nakwamba wakati umefika wa kuanzisha mamlaka ya kupinga vitendo vya udhalilishaji kama ilivyo kwa mamlaka ya kudhibiti dawa za kulevya ili kuipa mamlaka uwezo wa kufanya mambo yake yenyewe ikiwemo kuchunguza kesi na kupeleka mahakamani.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Husein Ali Mwinyi (kulia) akimkabidhi Tunzo Mkurugezi Mtendaji wa FCS, Francis Kiwanga (kushoto) kwa mchago wake katika kupinga ukatili wa kijinsia katika kongamano la harakati za kutokomeza vitendo vya udhalilishaji lilofanyika katika ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdulwakil Kikwajuni Zanzibar.

Dk. Mwinyi ameyasema hayo jana wakati wa kuipongeza Taasisi ya The Foundation for Civil Society (FCS) kwa mchago wake katika kupinga ukatili wa kijinsia katika kongamano la harakati za kutokomeza vitendo vya udhalilishaji lililoandaliwa na Taasisi ya ZEFELA inayofadhiliwa na FCS kujadili walipotoka, walipo na wanapokwenda lililofanyika katika ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdulwakil Kikwajuni Zanzibar.

Amesema haiwezekani yeye kama kiongozi anachukua juhudi za kupambana na vitendo hivyo huku baadhi ya watendaji wanakwamisha juhudi hizo na kubainisha kuwa inasikitisha kusikia viongozi aliowateua wanajihusisha na udhalilishaji.

“Jambo linalonisikitisha sana kwamba wateuzi ninaowateua nao wananiambia wanahusiana na udhalilishaji niwaaambie wananchi kwamba nimefanya kimakosa na nikibaini kwamba yupo mtendaji ambaye anafanya mambo haya basi sitasita kumchukulia hatua,” alibainisha.

Mkurugezi Mtendaji wa FCS Francis (katikati) akionesha Tuzo aliyokabidhiwa na Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Ally Mwiny (aliyesimama kulia) wakati wa Afla hiyo Visiwani Zanzibar. (kushoto) ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Raisi , Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora Haroun Ali Suleiman.

Hata hivyo, amesema anaendelea na dhamira yake ya kupambana na jambo hilo na kuhakikisha vitendo hivyo vinaondoka nchini na kwamba wananchi waliotoa maoni katika kongamano hilo wameonesha kuwa Taasisi zina jukumu la kupambana na vitendo hivyo.

“Ukiyasikia haya yanayosemwa hapa mimi binafsi Napata huzuni kubwa kwa sababu inaonekana Taasisi zanazotakiwa kufanya kazi zao hazifanyi na zina watu wanajulikana lakini wapo wanaendelea kutizimwa bila ya kuchukuliwa hatua,”alisema.

Dk. Mwinyi alisisitiza kuwa umefika wakati kila mtu kwa nafasi yake ajitathmini na kuwataka viongozi walikuwa chini yake kutoa taarifa kwa yale yote yaliyozungumzwa na wananchi katika kongamano hilo.

Aidha, Dk. Mwinyi aliongeza kuwa “Wapo wanaume ambao wanawapiga wake zao halafu wakija mnaambiwa kawaida tu lakini dini zinatuambia unapotaka kumpiga mke basi upo utaratibu unaotuelekeza,” aliongeza.

kuwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa FCS, Francis Kiwanga amemshukuru Rais Mwinyi kwa kutambua mchango wa Taasisi hiyo katika mapambano ya kupinga ukatili wa kijinsia Visiwani humo nakwamba watazidi kuunga mkono katika mapambano hayo.

Ameongeza kuwa tangu kuanzishwa kwa Taasisi hiyo mwaka 2002 imekuwa na uhusiano mzuri wa kufanya kazi na Asasi za kiraia na Serikali ya Zanzibar haswa Ofisi ya Msajili wa Jumuia za Kiraia Zanzibar ambapo kufikia sasa FCS inafanya kazi kama mshirika mkuu wa maendeleo mzawa kwa Jumuiya ya Kiraia ya Zanzibar inayosaidia karibu mashirika 16-20 kila mwaka.

“Miongoni mwa kazi kubwa iliyofanywa na FCS Zanzibar kwa miaka mitano (5) iliyopita ni pamoja na kutoa ruzuku yenye thamani ya Sh 4,094, 639,230 kwa mashiririka 73 yanayofanya kazi katika sekta za maboresho ya Sera, Haki za Ardhi kwa Wanawake, kupinga Ukatili kwa Watoto, Ushiriki na Ushirikishwaji wa Jamii katika maendeleo, Ajira kwa Vijana, Ujenzi wa Amani na Utatuzi wa Migogoro, kuchangia katika mchakato wa uaandaji wa rasimu ya Sheria ya NGOs kwa kufadhili zoezi la ukusanywaji wa maoni ya wadau na Jumuiya kutoka Pemba na Unguja,” amesema Kiwanga.

Mkurugezi Mtendaji wa FCS Francis (katikati) akitoa neno fupi la shukrani mara baada ya kupokea Tuzo hiyo kutoka kwa Rais Mwinyi (kushoto kwake), ni Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Ally Mwinyi ,na (kulia kwake) ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Raisi , Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora Haroun Ali Suleiman.

Ameongeza kuwa ili kuendana na kasi ya mabadiliko na changamoto za Ajira kwa vijana, FCS imekuwa ikifadhili nafasi za kujifunza kwa vijana waliotoka vyuoni kwenda kufanya kazi katika Jumuiya mbalimbali nakwamba jambo hilo limekuwa chachu ya kuongeza ujuzi katika kazi za jamii kwa vijana na kuwaunganisha na waajiri kutoka katika sekta ya AZAKI.

Nakuongeza kuwa: “FCS imeweza Kujenga na kuimarisha uwezo wa Jumuia za Kiraia Zanzibar kama mshiriki muhimu katika utungaji na utekelezaji wa Sera ikiwa ni pamoja na kuchangia moja kwa moja kwenye shughuli za kimaendeleo na katika kufanikisha hilo FCS imekuwa ikiwezesha mafunzo mbalimbali, kuanzisha Kituo cha Azaki Zanzibar Kujenga na kukuza mahusiano kati ya Jumuia za Kiraia na Serikali Zanzibar,” amesema Kiwanga.

Awali, akizungumza kwenye hafla hiyo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Raisi , Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora Haroun Ali Suleiman alisema vitendo vya udhalilishaji vinaumiza sana jamii ya Zanzibar.

Alisema serikali ya awamu ya saba iliunda kamati ya kitaifa ya kushughulikia mambo hayo lakini bado vyombo vinavyoshugulikia mambo hayo hazipo makini katika kushughulikia matendo ya udhalilishaji nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi kutoka Jumuiya ya Wanasheria Wanawake Zanzibar (ZAFELA) Jamila Mahmoud alisema kongamano hilo wana lengo la kujipima Asasi za Kiraia mambo wanayofanya katika kuondosha udhalilishaji.

Alisema bado hali ngumu katika masuala ya udhalilishaji na yanaendelea kuzidi kila siku Pamoja na jitihada mablimbali zinazochukuliwa na viongozi waliopita kwa kuhakikisha ifikapo mwaka 2022 Zanzibar iwe imeondokana na vitendo vyote vya udhalilishaji wa kijinsia.

Alisema kwa mwaka uliopita ZAFELA ilipokea kesi 100 hadi 150 na kuanzia Januari hadi Juni mwaka huu wamepoke malalamiko mapya 887 huku kituo cha huduma ya sheria wamepokea kesi zaidi ya 50 za watoto kukinzana na sheria.

Katika kongamano hilo Raisi Mwinyi alizindua mfumo wa kukusanya takwimu sahihi za mapambano dhidi ya udhalilishaji nchini.

Mkurugezi Mtendaji wa FCS Francis akizungumza wakati alipotoa hutuba yake mbele ya Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Ally Mwinyi mara baada ya kumalizika kwa zoezi la kupokea Tuzo katika ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdulwakil Kikwajuni Zanzibar.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles