24.8 C
Dar es Salaam
Sunday, April 28, 2024

Contact us: [email protected]

Nyimbo za Classical kupamba Tamasha la FFC Krismasi JNICC

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

DESEMBA 25 kila mwaka, Wakristo ulimwenguni kote usheherekea maadhimisho ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo zaidi ya miaka 2000 iliyopita.
 
Sherehe hizo maarufu kwa jina la Krismasi uwaleta pamoja wazazi, ndugu, jamaa na watoto kukaa pamoja kwa kula na kunywa huku wakipeana zawadi mbalimbali.


Katika kuadhimisha sikukuu hiyo kwa mwaka huu, Kwaya Flying Family inayojumuisha waimbaji kutoka madhehebu mbalimbali ya kikristo wenye vipaji vya uimbaji wameamua kumtukuza Mungu kwa njia ya uimbaji wa nyimbo zenye ufundi wa hali ya juu.
 
Kwa namna ya pekee tamasha la mwaka huu litaambatana na maadhimisho ya kusherehekea miaka mitano tangu kwaya hiyo ianzishe mwaka 2018.
 
Kwaya inajivunia kujenga umoja na upendo kwa wakristu kwa kutumia muziki na kuweza kuimba pamoja bila kujali tofauti zao za kimadhehebu kwa kipindi cha miaka mitano na kufanikiwa kuandaa matamasha makubwa sita yaliyowakusanya waumini na viongozi mbalimbali chini ya mchungaji mmoja Yesu Kristo.
 
Kwaya hiyo itafanya tamasha na wanakwaya wake kuimba ‘Classical music’ ambao ni maarufu duniani kote na umejizolea umaarufu tangu miaka ya zamani.
 
Innocent Fundisha ni Kiongozi wa kwaya hiyo anasema wapenzi wa muziki mtakatifu wakifika katika tamasha hilo ambalo linatarajiwa kufanyika Desemba 10, mwaka huu katika ukumbi wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNICC), jiini Dar es salaam watapata kusikia kazi za watunzi nguli kama George Handel, Wolfgang Mozart, Johan Bach, Joseph Haydn, Felix Mendelson, Anthonio Vivald na wengine wengi.
 
Anasema tiketi za tamasha hilo zinapatikana Kanisa Katoliki la St Peter Osterbay, Kanisa la Kiinjili na Kilutheri (KKKT) Msasani, Ofisi za Paones Posta Samora tower, KKKT Kijitonyama, Kanisa Katoliki Mwenge na Kanisa la Anglican Ilala.
 
Hata hivyo anasema pia wanatumia kazi za watunzi wazawa kama John Mgandu, Egidius Mushumbusi na Mathias Msafiri bila kusahau tenzi za rohoni.
 
Fundisha anasema si kazi rahisi kwa wanakwaya kujifunza nyimbo hizo lakini kwa msaada wa Mungu wanafanikiwa kushika na kujifunza kwa usahihi.
 
“Kwaya hii ilianzishwa Aprili, 2018 jijini Dar es Salaam ikiwa na wanakwaya wasiozidi 15 ila kwa sasa ina wanachama hai 40, tumeamua kumsifu Mungu na kutangaza sifa zake hapa duniani kwa njia ya uimbaji,” anasema Fundisha.
 
Anasema anatambua kuwa sikukuu ya Krisimasi uwaleta pamoja na ndugu, jamaa na marafiki hiyo anaamini kupitia tamasha hilo watu wataburudika, watafurahi na kudumisha utamaduni wa kusheherekea Krismasi kwa njia ya muziki wa classical.
“Tunatarajia kuwa na Askofu wa Kanisa Katoliki jimbo Kuu la Dar es Salaam, Thaddaeus Ruwa,ichi, Askofu wa Kanisa la Kiinjili na Kilutheri (KKKT) Dayosisi ya Mashariki na Pwani, Dk. Alex Malasusa, Askofu Jackson Sosthenes wa Kanisa la Anglican Dayosisi ya Dar es salaam.
 
“Pia tutakuwa na maaskofu wasaidizi Stephano Musomba na Henry Mchamungu wa Kanisa Katoliki jimbo kuu la Dar es Salaam, mapadre na wachungaji. pamoja nao tutakuwa na ushiriki wa viongozi wa serikali pamoja na viongozi wastaafu, wanadisplomasia wanaowakilisha nchi zao hapa nchini pamoja na washiriki kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania,” anasema
 
 Lengo la kwaya hiyo
 
Fundisha anasema lengo la kuanzishwa kwa kwaya hiyo ni kuleta umoja na mahusuano mazuri katika madhehebu ya kikristu kwa njia ya kushirikishana vipaji vya kimuziki.
 
“Tunashirikishana vipaji hivyo vilivyopo kwa kuandaa kwaya ya pamoja, matamasha mbalimbali, huduma kwa wahitaji pamoja na kushiriki matukio ya kijamii yanayolenga kudumisha umoja wa wakristu na taifa kwa ujumla,” anasema Fundisha.
 
Anasema kwaya hiyo yenye viongozi wa tano akiwa yeye ndiyo mwenyekiti imeanzisha bodi ya wadhamini yenye wajumbe tisa ambayo itazinduliwa Desemba 10, 2023 siku ya tamasha lao la Krismasi ikijumuisha viongozi maarufu kwa ajili ya kusimamia kwaya pamoja na kuweka mikakati bora ya kwenda mbele zaidi.
 
 Utendaji kazi wa kikundi
 
Anasema kwaya inafanya mazoezi mara moja kwa wiki siku ya jumapili kuanzia saa tisa alasiri hadi saa kumi na mbili jioni.
 
Aidha anasema sehemu kubwa ya mazoezi yanafanyika kwa njia ya mtandao wa Whatsup ambapo kila sauti ina kundi lake na walimu wa kuwasimamia siku zote za wiki na jumapili inakuwa ni siku ya kuunganisha tu.
 
“Mwalimu anajirekodi na kuwatumia, kisha kila mwanakwaya anasikiliza na kujifunza na kisha kujirekodi na kutuma tena kwenye group kwa ajili ya mwalimu kusikiliza na kurekebisha. Kwa sasa tumeenda mbali zaidi ambapo nyimbo nyingi wanakwaya wanasikiliza wao wenyewe kupitia mtandao wa Youtube.
 
“Kisha mwalimu wa kila sauti ukutana na kundi lake kwa ajili ya masahihisho kabla ya kwaya nzima kukutana na kuunganisha siku ya jumapili. Kwaya ina walimu kumi na moja wenye uwezo mkubwa wa kusoma muziki, kupiga kinanda na piano, utunzi wa kiwango cha juu kabisa pamoja kufundisha somo la muziki kwa wanakwaya na wasio wanakwaya,” anasema Fundisha
 
Anasema yote hayo yanafanyika chini ya kikosi imara cha wataalamu kikiongozwa na Mwalimu Wakili Nereus Mutongore, CPA Innocent Fundisha, Egidius Mushumbusi, Jerry Newman, Deogratias ngereza, Mathias Msafiri, Ainamringi Foya, Pauline Tumaini, Lucy Mutongore, Gloria Mugisha na Elizabeth Malenga.
 
Matarajio ya kikundi
 
Fundisha anasema matarajio ya kwaya hiyo ni kutambulika na kuheshimika kimataifa kupitia kiwango cha juu kabisa cha ubora wa muziki na matamasha yake na kwamba hayo yote yatatokana na mipango sahihi ya kujutuma na nidhamu ya hali yajuu katika kuishi malengo ya kwaya.
 
Wito kwa watu wengine
 
Anasema wanawashauri vijana kujituma muda na vipaji vyao kumtukuza Mungu kwani ndiye aliyewapa vyote walivyo navyo.
 
Fundisha anasema kupitia vikundi vya uimbaji wanamtukuza Mungu na kupata wasaa wa kuepuka kushiriki vitendo viovu huko mitaani hivyo upata baraka na neema kwa kufanya yampendezayo Mungu.
 
“Tunatoa wito kwa wakristu wote kutambua kuwa sisi sote ni kondoo na mchungaji wetu ni mmoja Bwana wetu Yesu Kristo, hivyo yatupasa kuishi kwa umoja na mshikamano na inawezekana kushirikiana bila kujali tofauti zetu za kimadhehebu.
 
“Lakini pia tunatoa wito kwa wenye vipaji vya kuimba au kupiga vyombo vya muziki wajiunge nasi kwa kufuata taratibu watakazopewa ili kudumisha umoja huu na kuueneza kwa wengi zaidi,” anasema
 
Hata hivyo anasema wanawashukuru wadau mbalimbali hasa walezi wao ambao ni maaskofu, wachungaji, mapadre pamoja na waamini kwa kuwapa moyo, kuwaongoza na kuwashauri, kuwawezesha kwa hali na mali bila kuwasahau Paones General trading ambao wanawafadhili kwenye matamasha yao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles