23.6 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Mwanafunzi afukuzwa kwa ushirikina

vifaa+vya+ushirikina

Na Ibrahim Yassin, Busokelo

UONGOZI wa Shule ya Sekondari Mwatisi Wilaya ya Rungwe mkoani Mbeya, umemfukuza mwanafunzi mmoja (jina tunalo) kwa madai ya ushirikina.

Mwanafunzi huyo anadaiwa kuhusika na kitendo cha baadhi ya wanafunzi shuleni hapo kukumbwa  na matatizo ya kuanguka na mapepo kwa muda wa miezi miwili mfululizo.

Mwanafunzi huyo pia anahusishwa na mzuka wa ajabu uliotokea hivi karbuni, ambapo ulikuwa ukianua vyakula vya watu wakati wakianika nje, huku ukiwakumba wanafunzi wa kike waliokuwa wakikimbilia porini na kuzua taharuki kwa wakazi wa eneo hilo.

Hali hiyo ilisababisha uongozi wa shule hiyo kuitisha mkutano wa hadhara  ulioshirikisha viongozi  wa  dini,  machifu na watu  wengine, lengo likiwa ni kufikia mwafaka  wa sakata hilo.

Furaha Mwakalundwa, Mwinjilisti  wa  Kanisa  la  Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Konde Jimbo la Mwakaleli, alisema kufukuzwa kwa mwanafunzi huyo hakuwezi kuleta tija kutokana na kwamba masuala ya ushirikina hayana uthibisho.

“Siku zote masuala ya ushirikina hayana uthibitisho, hivyo ni vyema hii kazi wangetuachia watumishi wa Mungu, ili tuendelee kuitatua kwa  nguvu za Mungu. Kumwondoa  mwanafunzi  huyo hatuwezi kujua kama kweli ni mhusika au laa,” alisema Mwakalundwa.

Baadhi ya wanafunzi walisema kuondolewa kwa  mwanafunzi mwenzao kumeleta faraja kutokana na hali hiyo kupungua kwa asilimia  90 ukilinganisha na awali.

“Alikua akiingia tu darasani au kila anapokutana na mwanafunzi yeyote walikuwa wakianguka na kupata kama kichaa na kuanguka na kusababisha  wanafunzi na walimu kumchukia,” alisema mmoja wa wanafunzi katika shule hiyo.

Walimu na wanafunzi walikuwa wakimwogopa na kumkimbia  kila anapoonekana ikiwamo kuogopa kumpatia adhabu  wakihofia kukumbwa na sintofahamu hiyo.

Ofisa Mtendaji wa Kata hiyo, Japhet Boniface, licha  ya  kukiri kuwepo kwa adha hiyo, alisema  kwa sasa hali iko shwari ukilinganisha na alipokuwepo mwanafunzi huyo.

“Vitendo kama hivyo vimekuwa vikijitokeza mara kwa mara kitu ambacho kinatupa wakati mgumu kujua ukweli wa jambo hilo,” alisema.

Mkuu wa  Shule hiyo, Eliza Halinga, alisema mwanafunzi huyo hajafukuzwa shule isipokua uongozi uliamua kumhamishia shule nyingine ili kunusuru hali yake kutokana na kila mwanafunzi kumchukia, hali iliyosababisha wanafunzi na walimu wengi kutofika  shuleni kwa hofu.

“Tuliamua kumwita mzazi wake ili kuongea nae ili tuweze  kumhamishia  shule  nyingine  kwani  kila  mwanafunzi  alikuwa  akimchukia  kutokana na kunguka kwao, pia licha  ya  kunguka  kwao  lakini kila akikutana na wanafunzi wenzake  walikuwa wakianza kuanguka na kujipigapiga,” alisema Halinga.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles