23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Dk. Shein amvaa Maalim Seif mkataba wa mafuta Z’bar

KHAMIS SHARIF- ZANZIBAR



RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema hajavunja Katiba wala sheria yoyote katika suala la utiaji saini mkataba wa mgawanyo wa uchimbaji wa mafuta na gesi Zanzibar kama ilivyodaiwa na baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa.

Kauli hiyo imekuja siku chache baada ya Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad, kudai mkataba wa utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi ulioitwa wa kihistoria na kutiwa saini Oktoba 23 mwaka huu ni batili.

Mkataba huo ulihusisha Kampuni ya Utafutaji na Uchimbaji Mafuta ya Rak Gas kutoka katika nchi ya Ras Alkhaimah ya taifa la Umoja wa Falme za Kiarabu (United Arab Emirates-UAE) na Zanzibar.

Dk. Shein alitoa taarifa hiyo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari mjini Zanzibar, baada ya kuwasili akitoka Nairobi nchini Kenya ambapo alihudhuria mkutano wa Kimataifa wa ‘Blue Economy’ wenye lengo la kukuza uchumi kupitia sekta ya uvuvi.

Alisema hakuna mgogoro wowote kikatiba ambao unahusu mkataba huo wa uchimbaji mafuta na kumtaka yule anaona kuwa suala hilo aende mahakamani ambapo ndipo sehemu  pekee inapopatikana haki.

Dk. Shein alisema serikali inapofanya maamuzi yoyote  hufanya kwa niaba ya wananchi hivyo hakuna sababu kwa baadhi ya viongozi wa kisiasa kueneza propaganda ambazo zinaweza kutoa dosari mkataba huo.

“Zanzibar imepitia dhoruba nyingi za maneno na wakati mwingine vitendo kutoka kwa wanasiasa hao. Hivyo kama wao wanatoa hoja hizo waachwe watoe naye kama msimamizi mkuu wa serikali aachwe afanyekazi kwa mujibu wa sheria.

“Tumeanza na hatua ya awali ya utafiti wa mafuta kwa upande wa Pemba hivyo ninaachofanya si kwa niaba yangu bali kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na wanancchi wake wote na si vinginevyo,” alisema Dk. Shein.

Rais huyo wa Zanzibar alisema katu hatengenezi mambo ya kumnufaisha binafsi bali husimamia kwa masilahi ya wananchi wote ili waweze kunufaika na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia ambayo itakuwa na manufaa kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Akizungumzia kuhusu utata wa kikatiba ambao baadhi ya viongozi wamekuwa wakiuhusisha na utiaji saini huo, Dk Shein alisema Tanzania Bara wana rasilimali zao na Zanzibar inazo zake hivyo hakuna sababu ya kuwapo kwa mivutano kutoka kwa viongozi.

“Zanzibar na Tanzania Bara na hata Jamhuri ya Muungano kwa ujumla, pande zote zitaendelea kuweka jitihada katika uchumi wa bahari hasa katika maeneo ya uvuvi, bandari, kilimo cha zao la Mwani pamoja viwanda ili kukuza na kuendeleza uchumi kwa lengo la kuwanufaisha wananchi kufaidika na rasilimali  zao.

“Tanzania ina rasilimali kubwa ya uchumi wa bahari ndogo ndogo, maziwa makubwa, mito pamoja na bahari kuu hivyo serikali inatarajia kuimarisha uchumi wake kupitia rasilimali hizi,” alisema Dk. Shein

Akizungumzia mikakati ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi,  alisema serikali kwa kiasi kikubwa inajipanga ili kutimiza lengoazma kutokomeza tatizo hilo.

Novemba 11, mwaka huu Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Shariff Hamad, alisema mkataba wa utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi ulioitwa wa kihistoria na kutiwa saini Oktoba 23 mwaka huu ni batili.

Alisema mkataba uliotiwa saini ni kwa ajili ya kugawana faida itayopatikana pindi uchimbaji wa mafuta au gesi utafanyika katika kitalu cha Zanzibar-Pemba (Production Sharing Agreement- PSA).

Maalim Seif alitoa sababu mbalimbali ikiwamo ya Muungano huku akiwataka Wazanzibar kuacha uvyama kuwa makini na suala hilo ambalo kwa namna moja ama nyingine alisema litakuja kuleta sintofahamu hapo baadaye.

“Hapa tuache uchama tuwe kitu kimoja si CUF, Chadema wala CCM lazima hili suala la mafuta na gesi liangaliwe kwa kuwa lina kasoro nyingi ikiwemo kutokuwa na uwazi.

“Suala la rasilimali ya mafuta na gesi lina umuhimu wa aina ya pekee kwa Zanzibar na watu wake kutokana na mazingira ya kikatiba, kisheria na kiuchumi hivyo basi bila ya kuwepo umakini, ukweli wa dhati wa wanaolisimamia na uwazi.

“Zanzibar, watu wake na vizazi vyao vya baadae watajikuta wameingizwa katika mgogoro mwengine mkubwa sana sawa au zaidi ya ule mgogoro wa mkataba wa Muungano,” alisema Maalim Seif kabla ya kusafiri kwenda nchi za Ulaya.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles