25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Bunge laridhia Mkataba wa Takwimu Afrika

Na Fredy Azzah -Dodoma



BUNGE limeridhia Mkataba wa Takwimu Afrika, huku kambi ya upinzani bungeni ikisema bila kufanyiwa marekebisho kwa Sheria ya Takwimu ya mwaka 2015, mkataba huo hautatekelezeka.

Hayo yalielezwa jana na Mbunge wa Momba, David Silinde (Chadema), alipokuwa akisoma maoni ya upinzani bungeni juu ya azimio la Bunge la kuridhia Mkataba wa Takwimu Afrika kwa niaba ya Waziri Kivuli wa Wizara ya Fedha na Mipango, Halima Mdee.

Alisema ili azimio hilo liwe na manufaa kwa Tanzania, ni vyema Serikali ikawasilisha sheria nyingine ya takwimu na kufuta ile ya 2015 na marekebisho yake ya 2018 ili ziendane na mkataba uliopitishwa.

“Pamoja na kufuta vifungu ambavyo kwa namna moja ama nyingine vinakiuka misingi ya haki za binadamu ikiwemo ya kupata na kupokea habari,” alisema Silinde.

Alisema wadau wa maendeleo wameona mapungufu ya Sheria ya Takwimu na marekebisho yake ya 2018 na baadhi yao wametishia kuondoa fedha za misaada ya kibajeti kwa Serikali.

“Kambi rasmi ya upinzani bungeni inaona kuwa hili ni jambo kubwa ambalo Serikali inatakiwa kuchukua hatua za dharura pamoja na kuwa tulishauri wafute vifungu hivyo ambavyo vinakiuka uhuru wa kutoa na kupokea habari pamoja na kupoteza na kuharibu dhana na umuhimu wa utafiti na takwimu,” alisema Silinde.

Alisema lengo la utafiti na takwimu ni kutafuta suluhisho la tatizo na si kushindana na Serikali, hivyo kambi ya upinzani inashangazwa na wasiwasi wa Serikali katika masuala ya takwimu.

Silinde alisema kambi hiyo inaona kuwa takwimu zitolewazo na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) zina mapungufu ambayo hawatakiwi Watanzania wayafahamu jambo linalokiuka azimio hilo.

SERIKALI YALIRIDHIA KWA MASHARTI

Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango akiwasilisha azimio hilo bungeni jana, alisema pamoja na kuridhia mkataba huo, Serikali itawasilisha maombi maalumu ili kuiwezesha Tanzania kutotoa taarifa za takwimu ambazo nchi itaona zina usiri na utolewaji wake unaweza kuathiri masilahi ya taifa.

“Utaratibu huu unatambuliwa kimataifa kupitia sehemu ya pili ya itifaki ya Vienna uliosainiwa mwaka 1969 ambapo Tanzania ni mojawapo ya nchi zilizoridhia kutumia mkataba huu tangu Aprili 12, 1976,” alisema Dk. Mpango.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles