27.2 C
Dar es Salaam
Thursday, May 2, 2024

Contact us: [email protected]

BASHE AZIFARIJI FAMILIA ZILIZOKUMBWA NA MAUAJI  

 

Na MWANDISHI WETU-NZEGA


MBUNGE wa Nzega Mjini, Hussein Bashe (CCM) amezitembelea familia ambazo wanawake watano wenye umri kati ya miaka 59 na 60 waliuawa kwa imani za ushirikina.

Wanawake hao wa Kijiji cha Undomo wilayani Nzega, waliuawa baada ya kuwapo uvumi kuwa walikuwa wakishiriki katika vitendo vya ushirikina na baadaye kukamatwa na baadhi ya wanakijiji na kuuawa kwa kupigwa mawe na kuchomwa moto.

Kwa sababu hiyo viongozi mbalimbali wakiwamo watendaji wa Serikali, walikamatwa   kulisaidia Jeshi la Polisi katika upelelezi.

Mpaka sasa zaidi ya watu 70 wanashikiliwa na polisi akiwamo diwani, mwenyekiti wa kijiji na viongozi wa sungusungu na baadhi ya wananchi katika kijiji hicho pamoja na wananchi.

Akitoa pole kwa mmoja wa waathirika hao, Bashe alilikemea tukio hilo huku akiwataka wananchi kutojichukulia sheria mkononi.

Aliviomba vyombo vya ulinzi na usalama wilayani Nzega kuanza kutoa mafunzo ya Polisi Jamii kwa sungusungu wote na kuweka utaratibu maalumu kuweza kuwafahamu na kuratibu shughuli zao nchini.

“Nitafanya mkutano wa hadhara utakaojumuisha wanakijiji wote na vyombo vya usalama kurejesha hali ya amani ambayo kwa sasa imepotea kutokana na kutanda hofu ya kamatakamata inayofanywa na polisi,”alisema Bashe.

Shughuli mbalimbali za uzalishaji na maendeleo zimesimama katika kijiji hicho kutokana na wananchi kuwa na hofu kubwa ya kukamatwa na  polisi.

Mikoa ya Kanda ya Ziwa na Kati imekuwa ikikumbwa na mauaji yanayotokana na imani za ushirikina huku waathirika wakubwa wakiwa ni wanawake na wazee (vikongwe).

Bashe ameendelea kuhubiri amani, upendo na ushirikiano baina ya wananchi katika kijiji hicho kwa kuwatembelea waathirika wote na kuzungumza na viongozi mbalimbali pamoja na wazee.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles