30.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 30, 2024

Contact us: [email protected]

Viongozi watatu CCM Ilala mbaroni kwa rushwa

CHRISTINA GAULUHANGA-DAR ES SALAAM

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Ilala imewafikisha Mahakama ya Wilaya ya Ilala vigogo watatu wa Chama cha Mapinduzi  (CCM) kwa kutuhuma za kuomba rushwa ya Sh  milioni tano kwa mfanyabiashara waweze kumpangisha katika kiwanja kimoja kinachomilikiwa na chama hicho Tawi la Amana Kata ya Ilala chenye namba 41 Y.

Akizungumza   Dar es Salaam jana, Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Ilala, Christopher Myava, alisema viongozi hao wamefikishwa katika Mahakama ya Ilala kwa mujibu wa  kifungu cha 15 ‘1’   ‘ a’  cha Sheria ya TAKUKURU na. 11/2007.

Aliwataja viongozi hao kuwa ni  Katibu wa Chama cha Mapinduzi Tawi la Amana, Jenifer Mushi,  Katibu Kata CCM Ilala, Devotha Bantulaki na Katibu Hamasa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Frank Joseph.

Myava alisema viongozi hao walikamatwa katika mtego wa rushwa baada ya kuomba Sh milioni tano ili wampangishe katika moja ya kiwanja kinachomilikiwa na CCM kata ya Ilala tawi la Amana.

Alisema  baada ya TAKUKURU kupokea taarifa waliweka mtego wa rushwa kwa   kuomba na kupokea  maeneo ya Klabu ya Wazee Ilala.

”Baada ya kuweka mtego Machi 22, mwaka huu ndipo tulipowanasa maeneo ya Klabu ya Wazee Ilala na Sekondari ya Msimbazi Ilala ambako watuhumiwa walikutwa na Sh milioni tatu walizopekea kutoka kwa mtoa taarifa,” alisema Myava.

Alisema CCM imekuwa na miradi mingi ambayo baadhi ya wanachama wasio waaminifu   wamekuwa wakijinufaisha nayo.

”Hadi sasa tuna kesi 22 za kuomba na kupokea rushwa za aina mbalimbali ambazo zipo mahakamani.

“Kama TAKUKURU tumejiimarisha kuwafikisha mbele ya sheria wote watakaobainika kujihusisha na vitendo hivi,”alisema Myava.

Watuhumiwa hao walifikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala Kinyerezi mbele ya Hakimu Mfawidhi, Martha Mpaze.

Awali, ilidaiwa na Mwendesha Mashtaka wa TAKUKURU, Veronica Chimwanda kuwa  Machi 21 mwaka huu,   kama Katibu wa CCM walimshawishi mfanyabiashara Daud  Kalaghe ambaye ni mmliki wa Daluni East Africa  Transport awape rushwa ya Sh milioni tano wampatie kiwanja kwa ajili ya biashara.

Ilidaiwa Machi 22, mwaka huu, Jenifer akiwa katibu CCM Tawi la Amana eneo la Msimbazi Sekondari alijipatia rushwa ya Sh milioni tatu mali ya Kalaghe kama kishawishi cha kumpatia eneo hilo.

Upelelezi   haujakamilika na  washtakiwa walikana shtka hilo hadi Aprili 8, kesi  itakapotajwa tena.

Washtakiwa Devotha na Joseph walipata dhamana kasoro Jenifer ambaye alirejeshwa mahabusu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles