Na MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM
MKURUGENZI wa ufundi wa TBL Group na viwanda vya SABMiller Kanda ya Afrika Mashariki, Gavin Van Wijk, amesema mkakati wa Serikali kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda unaweza kutekelezeka na kuleta maendeleo makubwa kwa nchi.
Alisema kinachotakiwa kufanyika haraka ni kujifunza kutoka nchi zilizofanikiwa katika sekta ya viwanda na kutumia mifumo ya uendeshaji viwanda kwa tija na ufanisi inayotumika katika nchi hizo ambayo imeziwezesha kuwa na viwanda imara.
Akiongea na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Wijk alisema kampuni ya TBL Group imeanza kuonyesha nia kuwa Tanzania ya viwanda inawezekana kutokana na viwanda vyake vya kutengeneza bia vilivopo nchini kuwa miongoni mwa viwanda bora vinavyoongoza barani Afrika kwenye mtandao wa viwanda vilivyopo chini ya kampuni ya SABMiller.
“Kwa miaka 6 mfululizo viwanda vya Tanzania vimekuwa vikishinda tuzo mbalimbali za ubora na kuwa tishio kwa viwanda vingine vilivyopo kwenye nchi nyinginezo za Afrika na mwaka huu rekodi ya kiwanda bora barani Afrika inashikiliwa na kiwanda cha TBL Mbeya, huku nafasi ya pili ikishikiliwa na kiwanda cha Mwanza, pia viwanda vya Arusha navyo viko kwenye nafasi za juu na bidhaa zinazotengenezwa na viwanda hivi ni tishio katika masoko ya kimataifa,” alisema.
Alisema siri ya mafanikio haya ni kuhakikisha mifumo ya kampuni ya uzalishaji yenye tija inafuatwa na matokeo yake ni kupatikana kwa uzalishaji wenye tija na viwango vya kimataifa.