23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Wazimbabwe waandamana kupinga bei ya mafuta

HARARE, ZIMBABWE

POLISI nchini Zimbabwe wamefyatua risasi hewani na kuwarushia mabomu ya machozi, watu waliokuwa wakiandamana mjini hapa kupinga kupanda maradufu kwa bei ya mafuta na hali mbaya ya uchumi.

Katika baadhi ya maeneo ya hapa na miji mingine waandamanaji walichoma matairi  na kuziba barabara baada ya muungano wa vyama vya wafanyakazi kuitisha maandamano.

Polisi waliwafyatulia risasi za moto waandamanaji katika eneo la Epworth, lililoko umbali wa kilomita 15 kutoka Harare.

Baadhi ya watu inadaiwa wameuawa na wengine kujeruhiwa na wengi kukamatwa ingawa idadi yao bado haijawekwa wazi.

Vurugu nchini Zimbabwe zimetokea siku moja baada ya Rais Emmerson Mnangagwa kupandisha zaidi ya mara mbili bei ya mafuta kutokana na ukosefu wa bidhaa hiyo.

Uamuzi huo ukaulazimisha Muungano wa Vyama vya Wafanyakazi kuitisha maandamano ya siku tatu na kusababisha biashara nyingi na shule kufungwa.

Msemaji wa muungano huo, Peter Mutasa  amesema hatua ya serikali inaonyesha kutoguswa na kujali kuhusu mwananchi masikini ambaye tayari amelemewa na majukumu chungu nzima.

Hata hivyo, Serikali imejibu maandamano kwa kuwatawanya polisi wa kupambana na ghasia huku helikopta za kijeshi zikionekana angani.

Kiongozi wa chama cha upinzani cha MDC, Nelson Chamisa, amesema maafisa wa usalama wanapaswa kujizua na kuwaacha wananchi kutumia haki yao ya kikatiba ya kuandamana kwa amani.

Ukosefu wa fedha taslimu Zimbabwe umeutumbukiza uchumi wa taifa hilo la Kusini mwa Afrika katika matatizo makubwa.

Hali hiyo inatishia kudhoofisha juhudi za Rais Mnangagwa za kurejesha uekezaji wa kigeni uliotengwa na mtangulizi wake Robert Mugabe.

Huku Ghasia zikiendelea Rais Emmerson Mnangagwa yuko Ulaya kwa ziara ya nchi tano ikiwamo Urusi pamoja na kuhudhuria kongamano la kiuchumi mjini Davos, Uswisi akijaribu kuwashawishi wawekezaji wa Kigeni kurudi kuwekeza Zimbabwe.

Hata hivyo, ziara hiyo imeshutumiwa nchini hapa, wakosoaji wake wakiwamo wa kambi ya Mugabe wakimtaka arudi nyumbani kutatua matatizo au ajiuzulu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles