23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Wizara ya Fedha yatoa somo mifumo ya kieletroniki

RAMADHAN HASSAN – DODOMA

TAASISI  za umma nchini zimetakiwa kuhakikisha zinapata ridhaa ya Wizara ya Fedha na Mipango na Wakala wa Serikali Mtandao (GePG) kabla ya kufanya ununuzi, uandaaji, usimamizi na utumiaji wa mfumo wowote wa kieletroniki wa usimamizi wa fedha za umma.

Hayo yalielezwa jana jijini hapa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango ,Dotto James wakati akifunga Mkutano Mkuu wa mwaka wa Watumiaji wa Mfumo wa Serikali wa Kieletroniki wa Ukusanyaji Mapato (GePG).  

Lengo la mkutano huo ni kuwajengea uwezo katika matumizi ya mfumo huo, wakala, taasisi na mashirika ya umma kanda ya kati ambapo pia katibu mkuu huyo alizindua mfumo wa GePG toleo la simu za mkononi (GePG App).

Alizitaka taasisi za umma nchini kutekeleza waraka namba tano wa hazina unaozitaka kuhakikisha zinapata ridhaa ya Wizara ya Fedha na Mipango na Wakala wa Serikali Mtandao kabla ya kufanya ununuzi, uandaaji, usimamizi na utumiaji wa usimamizi wa utumiaji wa mfumo wowote wa kieletroniki wa usimamizi wa fedha za umma.

“Napenda kusisitiza kuwa mfumo wa GePG kama ilivyo mifumo mingine ya kifedha inayoshughulika na miamala, inahitaji usuluhishi ufanyike kwa wakati hivyo nawaagiza nyote kuhakikisha mnafanya usuluhishi wa miamala inayopitia mfumo wa GePG kwa usahihi,”alisema.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Mifumo ya Usimamizi wa fedha kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, John Sausi, alisema kwa sasa mikakati yao ni kuhakikisha vibali mbalimbali vinapatikana kwa njia ya mtandao (online).

“Mfano mtu anataka kibali tunataka kila kitu amalize online lengo letu kila kitu kipatikane online na hili linawezekana kwa sababu tuna timu ya watalamu ambao wapo vizuri katika Wizara yetu ya Fedha na Mipango.

“Pia tunataka kuwezesha bili moja kulipa taasisi tofauti tofauti  mfano kwenye upatikanaji wa vibali, tunafikia control namba moja ilipe taasisi 10 na hii tunataka ndani ya mwaka huu wa fedha,”alisema.

Naye, mwakilishi wa mabenki, Domina Tarimo, alisema mfumo wa GePG umewasaidia kupunguza gharama za uendeshaji katika mabenki ambapo alisema wapo tayari kutoa ushirikiano kwa hali na mali.

Kwa upande wake, mwakilishi wa kampuni za simu, Arafat Ibrahim, alisema mfumo huo umesaidia kurahisisha mwingiliano wa makampuni ya simu, ulinzi, malipo kufanyika kwa wakati pamoja na usuluhishi kwa mteja.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles