MWILI wa mama wa Mhariri Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya New Habari (2006) Limited, Absalom Kibanda unatarajiwa kuagwa leo saa tatu asubuhi Masaki jijini Dar es Salaam.
Mama yake mzazi Kibanda, alifariki juzi katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), ambako alikuwa akiendelea kupatiwa matibabu baada ya kupatwa na ugonjwa wa kiharusi.
Akizungumza kuhusu msiba huo, Kibanda alisema mwili wa mama yake, Gwaseko Kapyela (76) utaagwa leo nyumbani kwake Masaki na baadaye kusafirishwa kwa ndege kuelelea wilayani Rungwe mkoani Mbeya kwa maziko.
“Mwili wa mama utaagwa hapa nyumbani kwangu Masaki saa tatu asubuhi na baadaye kupelekwa uwanja wa ndege muda wa saa sita mchana na utawasili jijini Mbeya jioni na baada ya hapo tutaanza safari ya kuelekea Rungwe kwa maziko siku ya jumamosi,”alisema Kibanda.