24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

MAWAZIRI WA JPM WAELEZA MIKAKATI MIPYA

Na ELIZABETH HOMBO-DAR ES SALAAM



MAWAZIRI na manaibu waziri walioapishwa jana na Rais John Magufuli, wameeleza mikakati watakayoanza nayo baada ya kuingia ofisini.
Mawaziri hao walieleza hayo baada ya kula kiapo Ikulu, Dar es Salaam jana.

KAIRUKI

Waziri wa Madini, Angellah Kairuki, alisema ingawa ni mgeni kwenye wizara hiyo atapambana na changamoto zilizopo kuhakikisha madini yanachangia vema kwenye uchumi wa taifa.
“Sijawahi kukaa kwenye wizara nyeti kama ya madini na nikiwa mwanamke wa kwanza kuongoza wizara hii najua kutakuwa na changamoto lakini nitapambana.

“Natambua madini ni injini ya uchumi hivyo nitaandaa mikakati ya namna gani sekta hii itakavyoongeza uchumi, nitakaa karibu na wawekezaji kwa sababu natambua Tanzania ina fursa nyingi za uwekezaji,”alisema Kairuki.
Alisema awali changamoto kubwa kwenye wizara hiyo ilikuwa ni mikataba mibovu lakini kwa sasa maboresho yamekwisha kufanyika.

“Wataalamu wangu watanieleza kilichofanyika nijue naanzia wapi…tutapitia sheria mpya ya madini na tutafanya kazi kwa mujibu wa sheria,”alisema.

Alipoulizwa namna alivyojipanga kukabiliana na changamoto zilizopo katika wizara hiyo ambayo mawaziri wamekuwa wakilazimishwa kujiuzuru kutokana na kashfa mbalimbali, alisema: “Ngoja niende, ni vigumu kujua lakini wacha niende.”
Wizara hiyo ilikua inaunganisha sekta za nishati na madini, lakini kwa sasa zimetenganishwa na kuwa wizara mbili tofauti.

KIGWANGALLA

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla, alisema akiingia ofisini ataanza na mambo ya matatu kuhakikisha wizara hiyo inasonga mbele.
Dk. Kigwangalla ambaye awali alikuwa Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo, Jinsia na Watoto, alisema atatumia muda mwingi kuwekeza katika kutangaza vivutio nchini.

Alisema eneo hilo limekuwa na changamoto nyingi ikiwamo rasilimali fedha.
“Nitaweka nguvu zangu na kuweka mbinu mpya kutangaza vivutio kwa sababu ni eneo ambalo limekuwa na changamoto nyingi. Pia nitamaliza mgogoro wa Loliondo mkoani Arusha… nitahakikisha unafika mwisho.
“Jambo jingine ambalo nitalishughulikia ni kupambana na ujangili,”alisema Dk. Kigwangalla ambaye pia ni Mbunge wa Nzega Vijijini.

JAFO

Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Suleimani Jafo aliwataka watumishi wote wa serikali za mitaa wajipange kufanya kazi kwa sababu hatakuwa na mchezo.
Pia aliwataka wakurugenzi na wakuu wa mikoa kusimamia mapato katika maeneo yao.

“Tamisemi ni wizara kubwa, niwaombe wakurugenzi, wakuu wa mikoa, wilaya na watumishi wote wafanye kazi kwa spidi ili tufikie malengo na huduma kwa wananchi.
“Watekeleze miradi vizuri katika maeneo yao na nidhamu na utendaji wa kazi ndiyo dira yangu,”alisema Jafo.

 

MKUCHIKA

Waziri Ofisi ya Rais- Utumishi na Utawala Bora, George Mkuchika, alisema atahakikisha watumishi wanakuwamo ofisini kuwahudumia wananchi kwa sababu baadhi yao wamekuwa wakitumia muda mwingi kunywa chai.
Akizungumzia mapambano dhidi ya rushwa, alisema atatumia muda wake mwingi kutoa elimu akishirikiana na Takukuru.
Mkuchika ambaye pia ni Mbunge wa Newala Mjini, alisema atazungumza na Waziri wa Elimu somo la rushwa lifundishwe kuanzia darasa la kwanza hadi chuo kikuu.

MPINA

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhanga Mpina alisema wizara hiyo ina changamoto nyingi hivyo atapambana kuzikabili.
“Wizara hii ina changamoto nyingi…ninajua Rais amenipa changamoto na mimi sijawahi kuchoka na sijawahi kuogopa,”alisema Mpina ambaye awali alikuwa Naibu Waziri wa Muungano na Mazingira.

UMMY

Waziri wa Afya, Maendeleo, Jinsia na Watoto, Ummy Mwalimu alisema changamoto iliyopo katika wizara yake ni saratani ya kizazi.
Alisema wagonjwa wanaosumbuliwa na saratani ya kizazi ni kwa asilimia 80 huku asilimia 12 ikiwa ni ya matiti.
“Ninatoa wito kwa Watanzania wawe na utaratibu wa kupima afya zao mara kwa mara kwa sababu asilimia 80 ya wagonjwa wenye ugonjwa huo wanaofika katika Hospitali ya Ocean Road wanakuwa na hali mbaya sana,”alisema.

 

LUGOLA

Naibu Waziri wa Muungano na Mazingira, Kangi Lugola, aliwatadharisha waliozoea kuvunja sheria ya mazingira wajue kuwa sasa amefika mlangoni.
“Nawaahidi Watanzania kwa sababu kwa muda mrefu yako maeneo ambayo wananchi wanakosa mvua matokeo yake wanakosa chakula kwa sababu ya uzembe kwa kukata miti.
“Sasa wajue kuwa nimepewa mdomo wa pili…na wale wanaotumia nguvu ya fedha wajue kuwa mwanamume ameingia lazima wafuate sheria,” alisema Lugola.

 

ULEGA
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega alisema atafanya kazi kwa nguvu na kasi kuhakikisha mifugo na uvuvi inafanikiwa.

 

MWANJELWA
Naibu Waziri wa Kilimo, Mary Mwanjelwa alisema: “Nimepewa imani na Rais na lazima nithibitishe imani hiyo kwa kuiweka katika matendo… tegemeo la Watanzania ni kila mmoja aweze kufanikiwa”.

 

MANYANYA
Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Stella Manyanya alisema atahakikisha Tanzania ya viwanda inafanikiwa na kuifikisha nchi katika uchumi wa kati.

 

AWESO
Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Jumaa Aweso alisema: “Haijawahi kutokea Wilaya ya Pangani kuteuliwa mtu, anayelala na mgonjwa ndiye anayejua tatizo, tutaomba ushirikiano wa dhati kwa kila mmoja”.

 

IKUPA
Naibu Waziri wa Tamisemi anayeshughulikia watu wenye ulemavu, Stella Ikupa, alisema atasimamia sheria ya walemavu na masuala ya watu wenye ulemavu.
“Sisi walemavu tuna changamoto nyingi kabla sijapata hii nafasi nilikuwa naipigia kelele hivyo nitahakikisha zile sheria na miongozo inatekelezeka,”alisema Ikupa.

 

 

NDUGAI AMSHUKURU KASHILILAH

Naye Spika wa Bunge, Job Ndugai alimshukuru aliyekuwa Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashililah kwa utumishi uliotukuka huku akisema hatamsahau.

“Ninyi mnatokana miongoni mwetu katika nyumba ile ya wabunge. Rais ameona awape nyadhifa hizi, kubwa na la kipekee nimkaribishe Katibu wa Bunge mpya, Stephen Kagaigai na kipekee nimshukuru Dk. Kashililah… asante sana kwa utumishi uliotukuka hatutakusahau,” alisema Ndugai.

Alisema ana imani na timu ya Baraza la Mawaziri na kwamba watafanya kazi vema.
“Mje Dodoma mmejiandaa, hii miaka miwili ya mwanzo walikuwa wanajifunzafunza, sasa tukienda Dodoma itakuwa ni kazi tu,” alisema Ndugai.

 

JAJI MKUU
Naye Jaji Mkuu, Profesa Ibrahim Juma alisema kile walichokitamka katika kiapo cha uadilifu wanapaswa kukizingatia kwa kufuata utaratibu wa sheria na Katiba kuepusha migongano.

 

KAGAIGAI
Katibu mpya wa Bunge, Stephen Kagaigai alisema majukumu yake yanajulikana yakiwa ni kufuata kanuni na sheria.
Hafla hiyo ya kuapishwa mawaziri na manaibu ilihudhuriwa na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, Spika wa Bunge, Job Ndugai, Jaji Mkuu, Profesa Ibrahim Juma, wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama na viongozi mbalimbali wa Serikali.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles