23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Majaliwa: Tunazungumza na mataifa mbalimbali yanunue korosho

Na RAMADHAN HASSAN-DODOMA

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali inaendelea na mazungumzo na mataifa mbalimbali yaweze kununua  korosho nchini.

Pia amesema vibali vya kuuza na kununua mahindi nje vipo na vinatolewa baada ya anayehitaji kufuata taratibu.

Kauli hiyo aliitoa jana bungeni alipokuwa akijibu maswali ya papo kwa hapo kutoka kwa wabunge.

Akiuliza swali, Mbunge wa Mtwara Mjini, Maftaha Nachuma (CUF) alitaka kujua Serikali ina tamko gani kutokana na bei ya korosho kuwa chini na wakulima kukataa kuuza zao hilo.

Akijibu, Waziri Mkuu alisema nia ya Serikali ilikuwa wafanyabiashara kununua korosho kwa njia ya minada kuleta ushindani wa bei.

Alisema pamoja na kuweka utaratibu huo bado bei hiyo imekuwa chini, hivyo Serikali inafanya mikakati mbalimbali kupandisha bei ya zao hilo.

Waziri Mkuu alisema pamoja na kuendelea kuzungumza na wadau mbalimbali, bado Serikali inaendelea na maongezi na mataifa mbalimbali waweze kununua zao hilo.

“Nawaomba wakulima wa zao hilo kuwa watulivu kwa sababu Serikali inaendelea kutafuta soko la zao hilo kama ilivyo kwenye zao la kahawa na mazao mengine,” alisema.

Akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Lucia Mlowo (Chadema) aliyetaka kujua nini tamko la Serikali kuhusu kukosekana kwa soko la mahindi licha ya wakulima kulima zao hilo kwa wingi, Majaliwa alikiri ni kweli kumekuwa na tatizo la soko.

“Waziri wa Kilimo alishatoa maelekezo kwa watendaji wake mbalimbali kuhusiana na uuzaji wa zao hilo nje ya nchi,” alisema.

Alisema kabla ya kuuza mahindi nje ni muhimu nchi kujua ina kiasi gani cha zao hilo ili kusiwe na upungufu ndani ya nchi baada ya kuuza zao hilo.

Majaliwa alisema kufuatia umakini huo ni vema mfanyabiashara aliyepata soko la nje kutoa taarifa kwa mkuu wa wilaya wa eneo husika ili naye awe na takwimu.

“Takwimu hizi ndizo zitatusaidia ni mauzo ya dola ngapi yamefanywa nje ya nchi,” alisema.

Akizungumzia kushushwa kwa bei ya pembejeo nchini, Majaliwa alisema hadi jana Serikali imeshaingiza tani 260,000.

Alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Neema Mgaya (CCM) aliyetaka kujua Serikali ina mpango gani katika kuwahamasisha wawekezaji kuwekeza nchini katika ujenzi wa viwanda vya mbolea kwani kwa sasa zaidi ya asilimia 90 inaagizwa kutoa nje ya nchi, alisema kwa sasa suala hilo linafanyiwa kazi ili kuwapo  mwagizaji mmoja badala ya kila mmoja kuleta binafsi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles