25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Kaseja atimuliwa Yanga

kasejaJUDITH PETER NA SAADA AKIDA
KLABU ya soka ya Yanga, imevunja mkataba wake na kipa, Juma Kaseja, kwa kushindwa kufuata kanuni na masharti yaliyowekwa na uongozi wa klabu hiyo, kuchelewa kuripoti kambini kwa saa 48 na kutohudhuria mazoezi.
Yanga ilitoa tahadhari kuwa mchezaji yeyote ambaye atashindwa kuripoti kambini ndani ya saa 48 na kukosa mazoezi bila ruhusa maalumu ya kocha, atakuwa amevunja mkataba wake na kujifukuzisha kazi.
Kaseja amekuwa mchezaji wa kwanza wa Yanga kukumbwa na adhabu hiyo ya kutimuliwa tangu kuanzishwa kwa sheria hiyo mpya iliyoanzishwa kwa lengo la kupunguza utoro kambini na vitendo vya utovu wa nidhamu.
Akizungumza na MTANZANIA jana kutoka Zanzibar ambako Yanga inashiriki michuano ya Kombe la Mapinduzi, Ofisa Habari wa timu hiyo, Jerry Muro, alisema uamuzi huo umefikiwa ili kukomesha tabia za utovu wa nidhamu pamoja na kuwataka wachezaji kufuata kanuni na sheria zilizopo ili kuepukana na sakata hilo.
Alisema tayari uongozi wa klabu hiyo umewapa taarifa wachezaji wake kuhusiana na jambo hilo huku ukiwataka kufuata taratibu zinazotakiwa ili kupata ruhusa ikiwa watakuwa na sababu ambazo zitapelekea kukosa mazoezi na kushindwa kufika kambini kwa wakati.
“Kama mchezaji amesajiliwa na Yanga ni lazima afuate sheria na kanuni zilizowekwa pamoja na kuhakikisha wanahudhuria mazoezi kila siku na kuingia kambini kwa wakati,” alisema.
Yanga ilitoa masharti hayo kwa wachezaji wake ili kukomesha tabia ya wachezaji wanaopenda kutegea kufanya mazoezi na kuchelewa kuripoti kambini bila kupata ruhusa maalumu jambo ambalo linadhihirisha utovu wa nidhamu.
Alisema Yanga imefikia hatua hiyo ili kuimarisha nidhamu ya wachezaji ambao imewasajili kwa ajili ya Ligi Kuu Tanzania Bara na ya Kombe la Shirikisho.
“Tunataka kuwa na timu yenye wachezaji wanaoongoza kwa nidhamu ili waweze kuwa mfano wa kuigwa na tunaamini mpango huu utasaidia kwa kiasi kikubwa kujenga timu imara yenye ushindani katika ligi kuu,” alisema.

Awali Yanga ilikuwa ikifundishwa na kocha raia wa Brazil, Marcio Maximo, aliyependa kusisitiza juu ya nidhamu kwa wachezaji wake tangu akiifundisha timu ya Taifa ‘Taifa Stars’, lakini kwa sasa inanolewa na Mholanzi, Hans Van Der Pluijm.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles