29.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 30, 2024

Contact us: [email protected]

Kamati ya Bunge yaitaka Serikali kufanyia maboresho mfumo kudhibiti upotevu wa mafuta

Na Nora Damian, Mtanzania Digital

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeshauri mfumo wa kielektroniki (Scada) unaosoma mita zinazopima mafuta uendelee kufanyiwa maboresho ili madhumuni ya kuanzishwa kwake yawezwe kufikia kiwango kinachotakiwa.

Mfumo huo ambao ulianza kusimikwa mwaka 2023 una lengo la kutatua tatizo la upotevu wa mafuta.

Akizungumza Februari 23,2024 baada ya kutembelea Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA) na kuona mfumo huo Mwenyekiti wa kamati hiyo, Dk. David Mathayo, amesema wamefurahishwa na uwekezaji ambao Serikali imefanya katika maeneo mbalimbali ambayo walipita.

Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini wakiangalia mfumo wa kielektroniki wa kudhibiti upotevu wa mafuta walipofanya ziara katika Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA).

“Baada ya mkandarasi kumaliza muda wake wa uangalizi umiliki wa Scada uwe chini ya Serikali, asiwe na ruhusu ya kutumia au kufungua mfumo kwa sababu hii ni siri ya mteja,” amesema Dk. Mathayo.

Kamati hiyo pia imeishauri Kampuni ya Kuhifadhi Mafuta (Tipper) isafishe zaidi matenki ambayo hayatumiki ili kuongeza uwezo wa kuhifadhi mafuta sambamba na kupunguza gharama.

Mapendekezo mengine ni kuhusu eneo la nyumba za Shirika la Maendeleo la Petroli (TPDC) litumike kujenga matenki mengine ya kuhifadhi mafuta ili meli zikija zishushe mafuta haraka na kuondoka.

Aidha imeshauri ulinzi uimarishwe katika mita za kupima mafuta (flow metre) kwa kujengwa uzio na kufungwa kamera za kisasa.

“Wafanyabiashara wa mafuta walindwe kuhakikisha wanakuwa salama na mikopo waliyokopa. TBS iweke vinasaba vya kielektroniki na magari yawekwe ‘seal’,” amesema Dk. Mathayo.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Felchesmi Mramba, amesema watafanyia kazi maelekezo yote yaliyotolewa na kamati hiyo na watawasilisha taarifa ya utekelezaji.

Wakala huo ulianzishwa mwaka 2015 ambapo ina majukumu ya kusimamia mfumo wa uagizaji mafuta kwa pamoja, kukusanya mahitaji ya mafuta na kutangaza zabuni kwa ajili ya kuleta mafuta nchini, kusimamia mikataba ya uagizaji mafuta na kuhakikisha mafuta yaliyoagizwa yanafika nchini kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa.

Majukumu mengine ni kuhakikisha mafuta ya kutosha yanakuwepo nchini wakati wote na kusimamia tararibu za uagizaji zenye ufanisi katika kuleta mafuta nchini.

Hadi kufikia Januari 2024 wakala huo umesajili kampuni za biashara ya mafuta (OMCS) 61

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles