24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Wanaolichafua gazeti la RAI kukiona

kibandaNA MWANDISHI WETU

KAMPUNI ya New Habari (2006) Ltd inayochapisha magazeti ya MTANZANIA, RAI, Bingwa, Dimba na The African, imelaani vikali, uzushi, uongo na upotoshaji wa hali ya juu unaofanywa na watu wasio na nia njema na kampuni hiyo.

Watu hao juzi walitengeneza mfano wa gazeti la RAI lenye ujumbe hasi na kulisambaza katika mitandao ya kijamii, likiwa na taarifa mbalimbali za uongo na uzushi ambazo haziuhusu uongozi wa kampuni hiyo na magazeti yake kwa ujumla wake.

Akizungumzia hali hiyo mjini Dar es Salaam jana, Mhariri Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya New Habari (2006) Ltd, Absalom Kibanda amesema ameshtushwa na hatua hiyo, lakini akawataka wasomaji na wafuatiliaji wa gazeti halisi la RAI kulipuuza gazeti hilo feki.

Alisema gazeti hilo linalosambazwa katika mitandao ya kijamii halina maana yoyote, kwani watu wanaofanya hivyo wamelenga kulichafua gazeti halisi kwa maslahi binafsi.

Alisema hiyo ni mara ya pili kwa watu hao wenye nia ovu na gazeti hilo, kutengeneza mfano wa gazeti la RAI na kulisambaza katika mitandao ya kijamii.

“Tumeshtushwa na hatua hii ya kurudia uovu wao, tulipoona kwa mara kwanza wametengeneza gazeti feki la RAI ambalo lina sura inayofanana na gazeti letu halisi na kuliweka katika mitandao ili kuwaaminisha watu kuwa gazeti linaloenda sokoni ndio lile ambalo lilikuwa na habari ambazo ni potofu zenye mwelekeo wa uchochezi, tulipuuza.

Hata hivyo wahusika wa uovu ule wa awali tuliwabaini.
“Watu hawa, wameurudia tena, sasa niseme inatosha, napenda kuwaambia wasomaji wa gazeti la RAI ambalo huchapwa kila Alhamisi kuwa, gazeti linalowekwa kwenye mitandao ya kijamii si gazeti halisi la RAI wala habari zile hazijawahi kuandikwa na RAI hata mara moja.

“Na hata ukizisoma habari zilizomo kwenye gazeti linalosambazwa mtandaoni zimetawaliwa na dhamira ya kulipaka matope gazeti halisi la RAI, wahariri na waandishi wake kwa malengo ambayo hatujayajua.

“Katika uchunguzi wetu tuliofanya baada ya gazeti feki kuwekwa mitandaoni kwa mara ya kwanza, tuliona kazi hiyo haramu inafanywa katika chumba kimoja cha habari ambacho watendaji na wahariri wake wana mrengo fulani wa kihabari.

Tulikaa kimya wakati ule wa kwanza kwa maana tuliamini wangejifunza kutokana na upuuzi wao.

“Lakini baada ya kuona wamerudia, tumeona kuna wajibu wa kuwajulisha wasomaji wetu ambao baadhi wanaingia kwenye mitandao ya kijamii kabla ya kusoma magazeti, kwamba kile ambacho wanakiona kwenye mitandao si gazeti halisi la RAI, gazeti la RAI linatoka kila siku ya Alhamisi ya kila wiki hata habari zinazowekwa kwenye gazeti hilo feki si za Alhamisi.

“Kutokana na hali hiyo tunaangalia namna bora ya kuwasiliana na mamlaka husika za kiserikali ili kupata njia sahihi ya kuwashughulikia hawa wanaokiuka sheria ya mitandao,” alisema.

Kibanda amewataka watu hao wenye nia ovu na kampuni ya New Habari (2006) Ltd, kuachana na mikakati yao hiyo miovu kwani haitawasaidia kufanikisha malengo yao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles