24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Nyalandu amaliza mgogoro Mbarali

NyalanduNA ELIUD NGONDO, MBEYA

WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, amemaliza mgogoro wa ardhi uliodumu karibu miaka 10 wilayani Mbarali, mkoani Mbeya.
Mgogoro huo unahusisha wakazi wa vijiji 21 waliotakiwa kuondolewa kwa madai ya kuvamia eneo la Hifadhi ya Taifa ya Ruaha.

Nyalandu, ambaye yuko ziarani mkoani Mbeya, jana alizungumza na wananchi na kuwahakikishia kuwa Serikali haiwezi kuwaacha wakiangamia.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliohudhuriwa na wakazi zaidi ya 15,000, alisema wananchi wanaoishi vijiji hivyo hawatahamishwa.

Alisema uamuzi huo ni utekelezaji wa maelekezo ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, kuitaka Serikali kuhakikisha inamaliza mgogoro huo.
Alisema kwa muda mrefu mgogoro huo umekuwa ukitafutiwa ufumbuzi wa kudumu na umefika wakati ni lazima mambo yafikie mwisho ili wananchi waendelee na shughuli zao za maendeleo.

“Naomba niseme kuwa vijiji vinavyotakiwa kuhama vitaendelea kuwepo na ninaagiza kufanyika kwa ukaguzi wa mpaka katika GN 28 ili kuhakikisha haki inatendeka katika suala hili. Huu mgogoro ni lazima ufike mwisho na uamuzi huu una baraka zote za Waziri Mkuu, Mizengo Pinda,” alisema Nyalandu.
Alisema maeneo yenye mgogoro mengi ndiyo kilimbilio na uchumi wa wananchi wa Mbarali kutokana na kuendesha shughuli za kilimo na makazi, hivyo Serikali haiwezi kuchukua uamuzi utakaokuwa na madhara kwa wananchi wake.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Mbarali, Mathayo Mwangomo, alisema mgogoro huo umeleta mpasuko mkubwa na kusababisha wananchi kukosa imani na baadhi ya viongozi.
Naye, Mbunge wa Mbarali, Modestus Kilufi, alisema mgogoro huo umedumu kwa miaka mingi na ilikuwa ni lazima mwafaka ufikiwe ili kuleta amani na utulivu ulioanza kutoweka.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles