22.4 C
Dar es Salaam
Friday, May 17, 2024

Contact us: [email protected]

Shule mpya Mnyamani yapunguza msongamano Vingunguti, Buguruni

Na Nora Damian, Mtanzania Digital

Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam imejenga shule mpya ya msingi ya Mnyamani na kupunguza adha ya msongamano katika shule zilizoko jirani nae neo hilo.

Kabla ya ujenzi wa shule hiyo watoto walilazimika kwenda kusoma katika Shule ya Msingi Buguruni, Vingunguti na nyingine hatua iliyohatarisha pia usalama wao kutokana na wengine kutembea kwa miguu.

Mwenyekiti wa CCM Kata ya Mnyamani, Mbaraka Mwinyimvua, akizungumza baada ya Mbunge wa Segerea, Bonnah Kamoli (Watatu kushoto), kutembelea Shule ya Msingi ya Mnyamani.

Akizungumza Januari 15,2024 wakati wa ziara ya kukagua miradi ya maendeleo Mbunge wa Segerea, Bonnah Kamoli, ameishukuru Serikali kwa kutoa fedha zilizowezesha ujenzi huo.

“Tunamshukuru sana Rais Samia na Serikali yetu kwa namna inavyoendelea kutekeleza miradi ya maendeleo kwa lengo la kuboresha na kusogeza huduma muhimu karibu na wananchi. Nawaomba muitunze na kuitumia vizuri miundombinu hii iliyogharimu mamilioni ya fedha za umma ili idumu kwa muda mrefu,” amesema Bonnah.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Kamati ya shule hiyo, Evelyn Mwakatuma, utekelezaji wa mradi huo umegharimu Sh milioni 306.9 hadi sasa.

Aidha amesema zaidi ya watoto 600 wa darasa la kwanza na awali wameandikishwa hatua iliyosababisha kushindwa kuandikisha watoto wa madarasa mengine.

Diwani wa Kata ya Mnyamani, Shukuru Dege, pamoja na kumshukuru Rais Samia kwa ujenzi huo ameomba fedha zilizotengwa kulipa fidia wananchi wawili waliogoma zielekezwe kununua eneo lingine ili kuongeza madarasa.

Zainabu Hashimu, mmoja wa wazazi wenye watoto wanaosoma katika shule hiyo ameishukuru Serikali kwa kujenga shule hiyo akisema itawaondolea adha watoto ya kusoma mbali.

“Watoto walikuwa wakivuka barabara kwenda shule na kuna wengine waligongwa, lakini kwa sasa wazazi tuna amani kwa sababu watoto wetu wanasoma karibu na hawalazimiki kuvuka barabara,” amesema Zainabu.

Mwenyekiti wa CCM Kata ya Mnyamani, Mbaraka Mwinyimvua, ameishukuru Serikali kwa kutekeleza mradi huo ambao umeondoa hofu ya usalama wa watoto wao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
587,000SubscribersSubscribe

Latest Articles