24.1 C
Dar es Salaam
Thursday, May 16, 2024

Contact us: [email protected]

MIFUPA YA BINADAMU YAPATIKANA BWAWANI

Na Kadama Malunde, Shinyanga


POLISI Mkoa wa Shinyanga, inafanya uchunguzi kuhusu tukio la kupatikana kwa mifupa inayodhaniwa kuwa ni ya binadamu katika Bwawa la Tinde lililopo Kijiji cha Nyambui Kata ya Tinde wilayani Shinyanga.

Mifupa hiyo inadaiwa kupatikana Oktoba 9 katika bwawa hilo wakati wananchi wa eneo hilo wakichimba kisima ili kupata maji ndani ya bwawa hilo ambalo limekauka kutokana na ukame.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, ACP Simon Haule, alisema  mifupa hiyo imebainika kuwapo katika eneo hilo wakati Diwani wa Kata ya Tinde, Jafar Kanolo (51), akikagua vyanzo vya maji na uharibifu wa mazingira.

“Wakati akiendelea na shughuli zake za kukagua vyanzo vya maji na uharibifu wa mazingira, diwani huyo aliwakuta wananchi waliokuwa wakitafuta maji kwa kuchimba katika bwawa hilo na ndipo alipogundua kuwapo kwa mifupa inayodhaniwa kuwa ni ya binadamu,” alieleza Kamanda Haule.

Alisema baada ya kupatikana kwa taarifa hizo, polisi ilifika katika eneo hilo kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa awali kwa kushirikiana na daktari mtaalamu wa viungo vya binadamu.

Aliitaja mifupa iliyopatikana katika bwawa hilo kuwa ni fuvu la kichwa, mfupa mmoja wa mguu sehemu ya paja, mfupa mmoja wa mguu chini ya goti, mifupa miwili ya mkono, taya moja ya upande wa chini, mfupa mmoja wa sehemu ya bega na mifupa 14 ya mbavu.

Kamanda Haule alisema uchunguzi zaidi kuhusu tukio hilo unaendelea ikiwa ni pamoja na kufuatilia na kupata taarifa kamili kutoka ofisi ya Mganga Mkuu Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga.

Pia alisema polisi inafuatilia kumbukumbu mbalimbali za polisi ili kuona kama kuna taarifa ya mtu yeyote aliyepotea au kufa maji bila kujulikana au kuuaw katika mazingira tatanishi.

Alisema hatua nyingine waliyoichukua ni kufungasha sampuli zote muhimu za mifupa hiyo kwa ajili ya kuipeleka kwenye ofisi ya mkemia mkuu wa serikali anayeweza kubaini vinasabana jinsia ya binadamu husika.

Aidha alisema uchunguzi wa awali unaonesha kuwa mifupa hiyo inadhaniwa kuwa ardhini kwa muda wa takribani miaka mitano iliyopita.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
587,000SubscribersSubscribe

Latest Articles