29.2 C
Dar es Salaam
Friday, May 17, 2024

Contact us: [email protected]

Japan yashirikiana na UNFPA kusaidia huduma za Afya ya Mama Kigoma

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

Ubalozi wa Japan nchini Tanzania na Shirika la Umoja wa Mataifa la Idadi ya Watu linaloshughulikia Afya ya Uzazi (UNFPA), leo Januari 31, 2024 wametia saini makubaliano ya ufadhili wa kusaidia shughuli za kuokoa maisha ili kuzuia vifo vitokanavyo na uzazi katika kambi za wakimbizi za Nyarugusu na Nduta katika wilaya za Kasulu na Kibondo pamoja na wananchi wenyeji waishio karibu na Kambi wa mkoa wa Kigoma.

Makubaliano haya yaliyotiwa saini yametengewa dola 359,964 (Sawa na Sh milioni 921) kwa ajili ya kusambaza bidhaa za afya ya uzazi katika kambi za wakimbizi na jamii inayowahifadhi wakimbizi na wakimbizi wenye ulemavu katika kipindi cha mwaka 2024.

Zaidi ya hayo, fedha hizo zitanunua vifaa muhimu vya matibabu na kutoa mafunzo kwa wahudumu wa afya walio mstari wa mbele ili kuhakikisha utoaji wa huduma bora za Afya ya Uzazi.

Mradi huu utawanufaisha zaidi ya watu 113,000, wakijumuisha wanawake, wasichana na wavulana waliobalehe pamoja na akina mama vijana (first time young mothers) na watu wenye ulemavu walioko kwenye kambi na nje ya kambi za wakimbizi mkoani Kigoma.

Katika hafla ya utiaji saini jijini Dar es Salaam, Yasushi Misawa, Balozi wa Japan nchini Tanzania, alisisitiza, “Japan imejikita katika kuboresha afya kwa watu duniani kote ili kuweza kufikia lengo la maendeleo endelevu la kuhakikisha kwamba watu wote duniani wanaweza kupata huduma za Afya,” amesema.

Japan imejikita zaidi katika maswala ya Afya. Ikiendeshwa na uongozi wake wa kimataifa katika utoaji wa huduma za afya kwa wote na sera yake ya usalama wa binadamu, Japan inawekeza katika miradi inayoboresha maisha ya wanawake na kulinda wanawake na watoto walioathiriwa na migogoro na majanga ya asili.

Mark Bryan Schreiner, Mwakilishi Mkaazi wa UNFPA katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amesema, “UNFPA iko mbioni kutoa huduma kwa wanawake na wasichana. Tunashukuru Japan kwakuweza kufadhili jitihada hizi, UNFPA inatoa huduma ya kuokoa maisha kwa wanawake na wasichana katika kambi za Nyarugusu na Nduta zinazosimamiwa na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kwa wastani, kambi za Nyarugusu na Nduta hushuhudia takriban mimba 2,004 kila mwezi, huku takriban wanawake 201 wakikumbana na matatizo ya Afya ya Uzazi na mimba kuharibika.

Wakati UNFPA na mashirika shirikishi yalifanikisha kutokomeza kabisa vifo vya akina mama katika kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu kwa mwaka 2022, wimbi la hivi karibuni la waomba hifadhi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo limeathiri zaidi miundombinu ya huduma za afya ndani ya kambi hizo.

Shida hii, pamoja na upungufu wa Huduma za Dharura za Uzazi (EmONC), Afya ya Uzazi (SRH),Huduma za Hedhi salama, na unyanyasaji wa kijinsia (GBV), huongeza hatari ya vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga na mimba zisizotarajiwa.

UNFPA inashirikiana na washirika wake wa utekelezaji wa jamii inayozunguka kambi za wakimbizi mkoa wa Kigoma, ambao ni Chama cha Msalaba Mwekundu Tanzania (TRCS), Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma (RAS Kigoma) na Borderless Tanzania Limited, kampuni ya kikundi ya Borderless Japan Corporation.

Msaada wa kifedha wa Japan unasisitiza kujitolea kwake kwa kudumu kushughulikia majanga ya kibinadamu kupitia lenzi ya usalama wa binadamu. Fedha hizi hupitishwa kupitia taasisi mbalimbali, ikiwemo UNFPA.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
587,000SubscribersSubscribe

Latest Articles