29.2 C
Dar es Salaam
Friday, May 17, 2024

Contact us: [email protected]

GBT yazindua na kukabidhi mradi wa maji Sekondari ya Kibaha

Na Gustafu Haule, Mtanzania Digital

BODI ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania (GBT) imezindua na kukabidhi mradi wa maji katika Shule ya Sekondari Kibaha mkoani Pwani wenye thamani zaidi ya Sh milioni 64 ikiwa ni sehemu ya kutatua changamoto ya ukosefu wa  maji katika shule hiyo.

Mradi huo umezinduliwa Oktoba 12, na Mkurugenzi  Mkuu wa Bodi hiyo, James Mbalwe, hafla ambayo pia imeshuhudiwa na Mkurugenzi wa Shirika la Elimu Kibaha, Robert Shilingi, walimu na wanafunzi.

Akizungumza mara baada ya uzinduzi huo Mbalwe amesema kuwa GBT ilipokea ombi kutoka katika Shirika hilo kuhusu uhaba wa maji katika Shule ya Sekondari Kibaha na hivyo kulipa kipaumbele .

Amesema baada ya kupokea maombi hayo GBT iliona kuna umuhimu wa kusaidia shule hiyo na hivyo kufanya jitihada za uchimbaji w na ujenzi wa tanki la ardhini la kuhifadhia maji lenye ujazo wa lita 100,000 pamoja na ununuzi wa matenki 10 yenye ujazo wa lita 10,000 kila moja.

Mbalwe amesema kuwa msaada huo umetolewa kama sehemu ya jitihada za GBT pamoja na wadau wake kusaidia jamii (CSR) katika nyanja mbalimbali lakini pia ni muendelezo wa kuunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Samia Suluhu Hassan.

Aidha, Mbalwe amesema kuwa pamoja na kusaidia mradi huo wa maji katika shule ya Sekondari Kibaha lakini pia GBT itaendelea kusaidia jamii katika kutatua changamoto mbalimbali za kielimu, afya, mazingira,Michezo na hata sekta nyingine.

“Tulipopata changamoto ya ukosefu wa maji katika Shule hii kubwa ya vipaji Bodi ya Michezo ya Kubahatisha haikusita kuja hapa na kuona namna ya kuwasaidia lakini leo tunafurahi kuona mradi huu mkubwa tumejenga na tunakabidhi kwa ajili ya matumizi ya watoto wetu,” amesema Mbalwe.

Amesema anatumaini kuona mradi huo utawezesha upatikanaji wa maji ya uhakika wakati wote na hivyo kutatua tatizo la muda mrefu la upatikanaji wa maji yasiyo ya uhakika hasa inapotokea hitilafu kwenye njia kuu za usambazaji wa maji.

Mbalwe ameomba kila mwana jumuiya wa Shule ya Sekondari Kibaha kuwa mlinzi na mtunzaji wa mradi huo ili uweze kusaidia vizazi vingi vijavyo hasusani wanafunzi wanaokuja kusoma shuleni hapo.

Mkuu wa Shule ya Kibaha Sekondari, George Kazi amesema kuwa changamoto ya ukosefu wa maji shuleni hapo ilikuwa inasababisha wanafunzi kukatisha masomo yao na kwenda kufuata maji maeneo ya mbali na shule.

Kazi amesema hali hiyo ilikuwa inasababisha wanafunzi kukosa molari wa kufuatilia masomo yao kwakuwa mara nyingi wanaporudi darasani huwa wamechoka na hivyo kushindwa kusikiliza vizuri yale yanayofundishwa darasani.

“Nachukue fursa hii kuishukuru Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania kwa hatua hii kubwa ya kutatua changamoto ya maji hapa shuleni kwani kwasasa wanafunzi wangu wanasoma vizuri na wala hakuna tena usumbufu wa kufuata maji wakati wa masomo,” amesema Kazi.

Mkurugenzi wa Shirika la Elimu Kibaha, Robert Shilingi, amesema mradi huo wa maji uliofadhiliwa na GBT ni mkubwa kwani umejumuisha kujenga uzio wa usalama kwenye tanki la maji,minara ya matenki na miundombinu ya usambazaji wa maji katika maeneo ya shuleni ikiwemo mabweni.

Shilingi, ameishukuru GBT kwa msaada huo ambapo pia ameomba Bodi hiyo kuendelea kusaidia katika kutatua changamoto nyingine zilizopo ndani ya Shirika hilo hasa katika kufanya marekebisho ya jiko la gesi ili kuweza kuondokana na shida ya kutafuta kuni kwa ajili ya kupikia chakula cha wanafunzi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
587,000SubscribersSubscribe

Latest Articles