HABARI njema kwa mashabiki wa Arsenal ni kwamba nyota wake watatu waliokuwa majeruhi, akiwamo Thomas Partey, wamerejea mazoezini.
Mbali ya Partey aliyekuwa akiuguza ‘enka’, mastaa wengine waliokuwa nje ya uwanja na sasa wameingia mzigoni ni Ben White na Gabriel Magalhaes waliofanya mazoezi ya pamoja jana.
Partey, raia wa Ghana mwenye umri wa miaka 28, hakuwa sehemu ya kikosi wakati Arsenal ikipoteza mechi zote tatu za msimu huu wa Ligi Kuu ya England (EPL).
Nyota huyo aliyeumia katika mechi ya mwezi uliopita dhidi ya Chelsea, amekuwa akiandamwa na majeraha tangu aliposajiliwa mwaka juzi akitokea Atletico Madrid lakini ni silaha muhimu kwenye eneo la kiungo anapokuwa fiti.