29.2 C
Dar es Salaam
Friday, May 17, 2024

Contact us: [email protected]

Kamati ya Bunge yaridhishwa na mradi wa Pori la Akiba Wami Mbiki

Na Beatus Maganja, Pwani

Kamati ya Kudumu ya Bunge, Ardhi, Maliasili na Utalii, imeridhishwa na utekelezaji wa miradi ya mpango wa Taifa wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na mapambano dhidi ya UVIKO – 19 iliyotekelezwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) ndani ya Pori la Akiba Wami Mbiki, Mkoani Pwani.

Akizungumza Januari 11, 2024 mkoani humo baada ya kutembelea na kukagua miradi hiyo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Timotheo Mzava amempongeza Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa ubunifu wake wa kutafuta fedha na maelekezo aliyoyatoa juu ya matumizi ya fedha za UVIKO ambazo zimeleta mapinduzi makubwa katika sekta ya utalii.

“Kwa mazingira na hali tuliyoiona katika Pori la Akiba Wami Mbiki, nadhani tutaungana sote kumpongeza kwa dhati kabisa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya kwenye nchi yetu lakini hasa kwa ubunifu mkubwa alionao wa kutafuta fedha lakini pia maelekezo aliyoyatoa juu ya matumizi ya fedha za UVIKO, ” amesema Mzava.

Aidha ameipongeza kamati yake kwa Wizara ya Maliasili na Utalii na TAWA kwa kazi nzuri waliyoifanya katika kusimamia miradi hiyo ambayo iligharimu zaidi ya bilioni mbili za Kitanzania.

VKamati hiyo imetoa wito kwa TAWA kuongeza mikakati ya kibiashara na kimasoko ikiwa ni pamoja na kutangaza hifadhi hiyo ili miundombinu iliyotengenezwa iweze kutumika kama ilivyokusudiwa na Serikali kupata tija inayotarajiwa.

Naye Naibu Waziri wa Malialisi na Utalii, Dunstan Kitandula amesema Wizara imejipanga kuhakikisha inaongeza jitihada katika kutangaza hifadhi hiyo ili kuongeza idadi ya wageni ikiwa ni pamoja na kutafuta wabia wa kushirikiana nao katika kuendesha shughuli za utalii na uwekezaji.

Awali akifafanua hoja zilizoibuliwa na baadhi ya wajumbe wa Kamati hiyo kuhusu mikakati ya TAWA katika kuchechemua utalii kwenye hifadhi ya Wami Mbiki, Kamishna wa Uhifadhi wa TAWA, Mabula M Nyanda amesema wamekuja na mpango mahsusi wa kufufua hali ya hifadhi hiyo kwa kumtafuta mwekezaji ambaye atawekeza kituo cha kuokoa na kulea wanyamapori wenye mahitaji maalumu (Wildlife Rescue and Rehabilitation Centre).

Amesema tayari TAWA imesaini mkataba na mwekezaji huyo ambao unatarajiwa kuleta manufaa makubwa kwa wanyamapori wenye mahitaji maalumu kama vile wagonjwa yatima, walionusurika katika matukio ya ajali na wanyamapori wanaotelekezwa na wazee wanaohitaji uangalizi maalumu.

“Uwepo wa kituo hichi katika hifadhi ya Wami Mbiki utakuza utalii wa ndani na wa nje kupitia program mbalimbali zitakazoendeshwa ikiwemo ya watalii wa kujitolea, utalii wa matukio lakini pia mwekezaji ameahidi kuleta wageni kati ya 30 hadi 50 kila mwezi jambo ambalo litachagiza utalii katika hifadhi hii,”amesema Nyanda.

Miradi iliyotembelewa na kukaguliwa na kamati hiyo ni pamoja na barabara yenye urefu wa kilometa 47.2, mabanda ya kulala wageni, lango kuu la kuingilia wageni linalojumuisha maduka ya kuuza bidhaa za utalii , jengo la kupumzikia wageni, jengo la kutoa taarifa kwa wageni, kituo cha mauzo, vyoo pamoja na nyumba za kuishi maofisa na askari watakaokuwa wakihudumia wageni.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
587,000SubscribersSubscribe

Latest Articles