Omary Mlekwa, Hai
Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya, mkoani Kilimanjaro, amewataka viongozi wa halmashauri hiyo kusimamia agizo la Rais John Magufuli la kutowatoza ushuru wa mazao wakulima na wafanyabiashara wadogo kwani suala hilo limekuwa likiwagandamiza Watanzania wanyonge.
Sabaya ametoa agizo hilo wakati akizungumza na wafanyabiashara katika soko la matunda na mboga mboga la Kwa Sadala ambapo aliwataka watumishi hao kuhakikisha wanaheshimu agizo hilo lililotolewa Aprili 29 mwaka 2016.
“Ni lazima agizo hilo lifanyiwe kazi na liheshimiwe, na endapo kutabainika mtumishi yeyote ataendelea kuwatoza ushuru wakulima hao wadogo hatua kali zitachukuliwa
“Lazima viongozi wote kuheshimu agizo la Rais wetu ambae ameamua kuwakomboa wakulima kwa kufuta ushuru hivyo tambueni kuwa kauli ya Rais ni Agizo,” amesema Ole Sabaya.
Akizungumzia suala la usafi katika soko hilo, ameitaka idara ya usafi na mazingira ya wilaya hiyo kuhakikisha kuwa wanazoa taka zote zilizoko katika soko hilo kabla ya Oktoba 9, mwaka huu ili kuepuka magonjwa ya mlipuko yanayosababishwa na uchafu.
“Mnachukua ushuru kwa watu hao lakini mnashindwa kuliweka soko katika hali ya usafi naagiza ifikapo siku ya Jumanne uchafu wote uwe umetolewa na mkishindwa msitoze ushuru kwa wafanyabiashara hawa,” amesisitiza Ole Sabaya.