Na Hadija Omary, Lindi
WANANCHI wa Kata ya Rutamba Halmashauri ya Manispaa ya Lindi, wameiomba Serikali kuongeza maofisa wanyamapori katika mtaa huo watakaosaidia kukabiliana na wanyama waharibifu kamaTembo ambao wamekuwa kero kwa kuharibu mashamba na mazao ya wakulima
Wakizungumza na Mtanzania baadhi ya wakulima waliohalibiwa mazao wamesema kuwa tembo hao wamekuwa wakifanya makazi katika mashamba yao kwani wamekuwa wakifanya uharibifu kwa zaidi ya siku saba sasa.
Nae Hamisi Abedi amesema tembo hao wanaendelea kula mazao ya wakulima kama vile mahindi, minazi, midizi, miwa na makabichi.
“Siku ya kwanza tembo hawa walianzia Miute wakala mpunga na minazi, siku ya pili wakala miwa na minazi wakang’oa siku ya tatu na ya nne wakaja tena ,siku ya tano ndo wakatoka Miute wakafika Chiti wakala minazi, mahindi, ndizi, kutoka hapo wakaenda kulala jiona yake wakaja tena.
“Yaani leo ni siku ya saba wanaendelea tu kuja hata hivyo huwenda wakaja kwa sababu wakitoka hawaendi mbali ikifika tu wakati wa jioni wanarudi tena mashambani,” amesema Abedi
Nae Rashidi Tendaga amesema kuwa uharibifu uliofanywa na tembo hao katika shamba lake ni mkubwa na kulingana na umri wake hataweza tena kuanzisha shamba kama hilo la minazi kwani mpaka kuja kupata mazao uchukua muda mrefu
” Zao la nazi hadi kupata mavuno ni miaka 15 mpaka 17, mimi mwenyewe nimepanda minazi mwaka 1976 nimeanza kuangusha hivi karibuni, hili ni pigo sana kwa wakulima tulio wengi maana hata ukianzisha shamba jipya leo uwezi kuvuna karibuni” amesema Tendaga
Kwa upande wake mtendaji wa mtaa huo, Chilala Ngallya amesema kuwa hadi sasa takwimu za awali zilizofika katika ofisi yake ni wakulima 13 ndiyo walioathiriwa mashamba na mazao yao na tembo hao.
Amesema uharibifu huo ni pamoja na minazi 285 migomba 322 , matikiti 3000 ,mpunga heka moja , nyanya heka moja huku akieleza kuwa idadi hiyo huwenda ikaongezeka kutokana na tembo hao kuendelea kuwepo katika maeneo hayo
Naye mwenyekiti wa mtaa wa huo, Nurudin Simba, amesema kwa njia inayotumika kuwafukuza tembo hao huwenda isizae matunda kwa kuwa maofisa wanyamapori wanaowategemea wanatoka katika kata jirani ambako na huko pia wapo tembo ambao wanahangaika kuwafukuza ili wasiendelee kuvamia mashamba ua wakulima
“Mimi kama mwenyekiti wa mtaa huu ninaiomba serikali iongeze nguvu ya maafisa wanyamapori tena ikiwezekana waanzishe kituo katika kata hii ili kukabiliana na wanyama hawa vinginevyo wakulima hawa wataendelea kupata hasara pasipo sababu za msingi,” amefafanua Simba.