27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Neymar atia hofu Brazil

RIO DE JANEIRO, BRAZIL 

SIKU chache baada ya kuvuliwa unahodha katika timu ya taifa ya Brazil, mshambuliaji wa timu hiyo, Neymar, ametia hofu baada ya kuumia goti wakati wa mazoezi ya timu hiyo kuelekea michuano ya Kombe la Copa America.

Brazil ni wenyeji wa michuano hiyo msimu huu ambapo inatarajia kuanza kutimua vumbi Juni 14 hadi Julai 7, mwaka huu kwa timu 12 kutoka Amerika ya Kusini zikioneshana ubabe kwenye miji mitano.

Neymar aliumia wakati wa mazoezi ya pamoja juzi Jumanne na alionekana akitoa machozi huku akiugulia maumivu ya goti la kushoto. Hata hivyo, hakuweza kuendelea tena na mazoezi na alitolewa moja kwa moja nje.

Nyota huyo ambaye anakipiga katika klabu ya PSG, aliungana na daktari wa timu hiyo, Rodrigo Lasmar, kwa ajili ya kwenda kufanyiwa matibabu. Mchezaji huyo ameumia ikiwa ni siku moja baada ya kuvuliwa unahodha.

Katika michuano ya Kombe la Dunia mwaka jana nchini Urusi, Neymar alitajwa kuwa nahodha wa kudumu katika kikosi hicho cha Brazil chini ya kocha wao Tite, lakini sasa nafasi hiyo inachukuliwa na nyota mwenzake wa PSG, Dani Alves kuelekea michuano hiyo.

Inasemekana kuwa Neymar amevuliwa kitambaa hicho kutokana na utovu wa nidhamu ambao anahusishwa nao. Wiki kadhaa zilizopita mchezaji huyo baada ya kuonekana akimshambulia shabiki wa timu ya Rennes, hivyo chama cha soka nchini Ufaransa kilimpa adhabu ya kufungiwa michezo mitatu.

Hata kabla ya adhabu hiyo kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, mchezaji huyo alifungiwa michezo mitatu na Chama cha Soka barani Ulaya (UEFA) kutokana na kauli chafu kwa mwamuzi wa mchezo kati ya PSG dhidi ya Manchester United kwenye mchezo wa pili wa hatua ya 16 bora kwenye Uwanja wa Parc des Princes.

Kutokana na baadhi ya sababu kama hizo, kocha huyo wa Brazil ameamua kumvua unahodha mchezaji huyo ikiwa ni wiki moja kabla ya kuanza kwa michuano hiyo ya Copa America. 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles