MWILI wa aliyekuwa mwanamuziki wa kizazi kipya, Michael Denis maarufu kwa jina la Joni Woka, unatarajiwa kuzikwa leo katika makaburi ya Sahare mkoani Tanga.
Mwakilishi wa waanii, Fredrick Mariki maarufu Mkoloni, alisema kifo cha Joni Woka kimetokana na kuangukiwa na kitu kizito wakati alipokuwa akitengeneza gari kisha akakimbizwa katika Hospitali ya Sinza kisha akahamishiwa Taasisi ya Mifupa na Mishipa ya Fahamu (Moi) hadi mauti yalipomfika.
John Woka alikuwa msanii wa kundi la Watukutu, alianza kung’aa aliposhirikishwa katika nyimbo za kundi la Wagosi wa Kaya mwaka 2001.
John Woka amezaliwa mwaka 1981 Tanga, ameacha mke na mtoto mmoja.
Naye Katibu Mtendaji wa Basata, Godfrey Mngereza, amewataka wasanii waendeleze ushirikiano na kuacha makundi si tu wakati wa misiba.
“Muige mambo mema aliyoacha John Woka ikiwemo kuthamini kazi zake kwa kuwa kifo hakina wakati maalumu wote tujiandae kwa kuendeleza mema,’’ alimaliza.
Naye Keisher aliwataka wasanii kuiga mambo mema aliyoacha msanii huyo badala ya kuendekeza mambo yasiyofaa kwa jamii.
Wasanii mbalimbali walijitokeza katika kuaga mwili wa msanii huyo.