MWANAUME raia wa Vietnam amehukumiwa kifungo cha miaka mitano gerezani baada ya kubainika kusambaza kwa makusudi virusi vya Corona.
Mahakama ilimkuta na hatia bwana Le Van Tri ilipojiridhisha kuwa aliwaambukiza Corona watu nane na mmoja kati yao alipoteza maisha.
Awali, Vietnam ilionekana kuidhibiti vilivyo Corona lakini kasi ya maambukizi ilizidi kuanzia Juni na hadi sasa waathirika ni 530,000 huku zaidi ya 13,300 wakipoteza maisha.
Kwa mujibu wa kile kilichoelezwa na Mahakama, sehemu ya watu ambao Tri aliwaambukiza ni ndugu zake na adhabu ya kifungo itakwenda sambamba na faini ya Dola za Marekani 880 (zaidi ya Sh mil. 2 za Tanzania).