Na JANETH MUSHI-ARUSHA
WANAFUNZI watatu wa Shule ya Msingi Nafko, wamefariki dunia baada ya kulipukiwa na kitu kinachodhaniwa kuwa ni bomu katika wakatu wakilisha mifugo karibu na eneo la JWTZ wilayani Monduli.
Akizungumza na MTANZANIA jana Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Nafko, Kata ya Loksale wilayani humo, Neiman Silas, alisema kuwa tukio hilo lilitokea Septemba 15, mwaka huu wakati watoto hao wakichunga mifugo.
Aliwataja watoto hao kuwa ni Daya Silangei, Sam Nyangusi na Landisi Saitabau, ambapo siku ya tukio watoto hao walikuwa wakichunga mifugo katika malisho ya kijiji, ambapo ni karibu na eneo wanalifanyia mazoezi JWTZ.
“Ni kweli kuna tukio limetokea hapa kijijini, ajali hiyo imetokana na mabomu yanayorushwa na wanajeshi kipindi wanafanya mazoezi kwenye eneo la jirani bahati mbaya yakapitiliza yakaingia kwenye makazi ya watu.
“Watoto walikuwa wakichunga mifugo eneo la upande wa malisho ya kijiji, sio upande wanapofanyia mazoezi wanajeshi na kwa bahati mbaya inadaiwa walikuwa wanalichezea linawalipukia wakafa wote na maandalizi ya maziko yanaendelea, watazikwa leo,” alisema
MTANZANIA ilimpomtafuta Kamanda wa Polisi Mko wa Arusha, Charles Mkumbo, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo saa 4 asubuhi ambapo uchunguzi unaendelea.