27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

JET YAMKAANGA MWEKEZAJI KILWA

Na MWANDISHI WETU-DAR ES SALAAM

CHAMA cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania (JET), kimeiangukia Serikali kupitia Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi kuingilia kati urejeshwaji wa ardhi ya wananchi wa Mavuji, Migeregere, Naikokwe na Liwiti Wilaya ya Kilwa, ambayo imechukuliwa na mwekezaji na ameshindwa kuiendeleza kwa muda wa zaidi ya  miaka 10.

Kutokana na hali hiyo inadaiwa kuwa mwekezaji huyo Kampuni ya Bioshape Tanzania Ltd baada ya kushindwa kuiendeleza ardhi hiyo hivi sasa yupo katika harakati za kuikabidhi ardhi hiyo kwa mwekezaji mwingine kinyume cha utaratibu.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya JET, Leah Mushi, alisema katika utafiti wao walioanya kupitia timu ya wanahabari wilayani Kilwa imebainika kuwa wananchi kwa sasa wanashindwa kuendelea na shughuli za kilimo kutokana kukosa maeneo ya kilimo.

Alisema baada ya kuzungumza na wananchi na kwa mujibu wa mikataba ambayo Kampuni ya Bioshape Tanzania kwa kupewa hekta 64,000 za vijiji vine na Serikali ya Mkoa wa Lindi mwaka 2006 lakini hadi sasa bado eneo hilo halijaendelezwa jambo ambalo ni kinyume cha sera ya uwekezaji Tanzania.

“Sisi JET tunaamini kwamba kupitia Serikali yetu sikivu ya awamu ya tano chini ya Rais Dk. John Magufuli kwa kusaidiwa na Waziri wa Ardhi, William Lukuvi, watalifuatilia kwa kina suala hili kama wanavyofanya kwa mikoa ya Morogoro na Tanga.

“Hata wakati mwekezaji huyu anapewa eneo hilo hakuna tathimini yoyote ya athari za mazingira iliyofanywa kuhusu kilimo cha mibono kwani hata ilionekana pia ilibainika kuwa na matatizo jambo ambalo lilifanywa na maofisa wasiokuwa waaminifu wa NEMC,” alisema Leah.

Kutokana na hali hiyo alisema kwa sasa wananchi wanaiomba Serikali iwarudishie ardhi yao ili waweze kuitumia kwa ajili ya shughuli za kilimo ambapo kwa sasa hulazimika kutembea umbali wa zaidi ya kilometa 10 kufuata mashamba ya kilimo jambo ambalo ni hatari kwa maisha yao.

“Mahitajiya ardhi kwa wananchi yameongezeka hasa kwa ajili ya kilimo, ufugaji. Kwa sasa baadhi ya familia za wakulima hutembea kilometa nane kwa siku ili kwenda shambani na wakati wa masika hulazimika kukamia huko, jambo ambalo limesababisha baadhi ya watoto kuacha shule,” alisema

Naye mmoja wa timu ya wanahabari waliokwenda kwa ajili ya kufanya utafiti huo wilayani Kilwa, Jimmy Charles, alisema Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) bado kinaendelea kumtambua mwekezaji huyo aliyeshindwa kutimiza wajibu wake kwa mujibu wa sheria za nchi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles