24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Yanga ya kwanza robo fainali FA

nonga msuvaNA JENIFFER ULLEMBO, DAR ES SALAAM

TIMU ya Yanga jana ilifanikiwa kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya maafande wa JKT Mlale, katika mchezo wa hatua ya 16 bora ya Kombe la FA uliochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mabao ya ushindi ya Yanga yalifungwa na Paul Nonga na Thaban Kamusoko, lakini ‘assist’ za mabao hayo yote zilitoka kwa Geofrey Mwashiuya aliyesajiliwa na Yanga kutoka Mbeya City katika kipindi cha usajili wa dirisha kubwa mwaka jana.

Mwashiuya amerudi katika ‘headlines’, baada ya Jumamosi iliyopita pia kutoa pasi ndefu safi kwa Amissi Tambwe ambaye alifunga bao la pili na kuwazamisha mahasimu wao Simba katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliowakutanisha watani wa jadi Simba na Yanga ambapo Wanajangwani walichomoza na ushindi wa bao 2-0.

Yanga imekutana na JKT Mlale baada ya kuwatandika Friends Rangers bao 3-0, mchezo uliochezwa Januari 22 mwaka huu.

Katika mchezo huo wa jana, JKT Mlale ndio walikuwa wa kwanza kuona lango la Yanga, baada ya kufunga bao la mapema katika dakika ya 20 mfungaji akiwa Mgandila Shabani, baada ya kutumia vema uzembe wa mabeki wa Yanga na kuachia shuti kali ndani ya 18, lililoenda moja kwa moja wavuni.

Yanga walianza mchezo huo taratibu huku wakionekana kuidharau JKT Mlale, ambapo katika dakika 10 za mwanzo Msuva alipoteza nafasi mbili za kufunga.

Baada ya JKT Mlale kupata bao hilo, Yanga walizinduka na kuzidisha mashambulizi ambapo walipata bao la kusawazisha dakika ya 37, kupitia kwa Nonga alieitendea haki krosi ndefu ya Mwashiuya.

Kipindi cha pili kilianza, Yanga walifanya mabadiliko alitoka Matheo Anthony na nafasi yake kuchukuliwa na Donald Ngoma, huku dakika ya 50 JKT Mlale nao walifanya mabadiliko kwa kumtoa Alex Seti na nafasi yake kuchukuliwa na Raphael Siame.

Dakika ya 58, Kamusoko aliyeingia kuchukua nafasi ya Salum Telela ‘Abo Master’, aliyeumia dakika ya 54, aliipatia Yanga bao la pili na la ushindi akiunganisha vema pasi ndefu ya Mwashiuya ambaye amerudi kwa kishindo.

Yanga walifanya tena mabadiliko dakika ya 63 kwa kumuingiza Malimu Busungu kuchukua nafasi ya Nonga, huku mchezaji wa JKT Mlale, Othuman Muhagame, alionyeshwa kadi ya njano kwa kumfanyia madhambi Busungu aliyeingia.

Yanga: Deogratius Munishi, Mbuyu Twite, Osker Joshua, Kelvin Yondani, Nadir Haroub, Said Juma, Simon Msuva, Salum Telela, Matheo Anthony, Paul Nonga na Geofrey Mwashiuya.

JKT Mlale: Noel Murish, Lucas Chapanga, Gerimanus Chindera, Said Ngapa, Frank Tesha, Othuman Muhanga, Mgandila Shabani, Omari Mnubi, Richard Mwadiga,Edward Songo na Alex Seri.

Mwamuzi: Israel Mjuni.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles