NA BRIGHITER MASAKI, Mtanzania Digital
SERIKALI kupitia Bodi ya Filamu Tanzania, imezindua rasmi tuzo za filamu zilizopewa jina la Taffa, huku watayarishaji na waandaaji wakitakiwa kutengeneza kazi zenye maadili.
Akizungumza na waandishi na wadau wa filamu nchini, Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa, amesema kupitia Selikali ya Rais Samia Suluhu Hassan, inaleta tuzo ya filamu kwa mara ya kwanza.
Bashungwa amesema tuzo  hizo zitakuwa ni endelevu na zitasimamia haki kwa kuwa zitaongeza hamasa katika tasnia ya filamuna  na mwaka huu zitajikita kutazama upungufu ili kwa miaka ijayo ziwe  na ubora mkubwa.

Hata hivyo Bashungwa ameeleza kuwa serikali imefanikiwa kuziweka katika eneo moja Taasisi za Bodi ya Filamu, Cosota na Baraza la Sanaa (BASATA) ili kurahisisha upatikanaji wa huduma za wadau wa sanaa ambapo taasisi hizo zipo kwa sasa Kivukoni Jengo la Utumishi jijini Dar es salaam.
Kwa upande wake Katibu Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Filamu, Kilonzo Kiagho amefafanua moja ya malengo kuanzisha tuzo hizo ni kutambua mchango wa wanatasnia wa filamu wanaofanya kazi nzuri ili kuongeza chachu katika sekta hiyo.
“Wasanii watembee kifua mbele wajitokeze kwa wingi kufanya uwasilishaji wa filamu zao kwani mwisho wa kukusanya ni Septemba 26, mwaka huu na mchakato huo umeanza rasmi na tupokea kazi katika ofisi za bodi ya filamu,” amesema.
Kiagho amefafanua zaidi kuwa tuzo hizo hazina upendeleo zina vipengele ambavyo wasanii wataweza kutuma ushiriki wao, fainali ni Novemba 6, 2021.
Miongoni mwa vipengele vinavyoshindaniwa ni msanii anaechipukia wa kike na kiume,mchekeshaji bora wa vichekesho wa kike na kiume, filamu bora ya mwaka.