25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

“Udiwani sio ajira, anzisheni miradi binafsi ya kiuchumi”-Makungu

Na Allan Vicent, Tabora

Madiwani Mkoani Tabora wameshauriwa kuwa na vyanzo binafsi vya mapato ili waweze kufanikisha utekelezaji majukumu yao pasipo kuathiri maisha ya familia zao.

Ushauri huo umetolewa juzi na Katibu Tawala wa Mkoa, Msalika Makungu alipokuwa akizindua vikao vya Baraza la madiwani wa Halmashauri ya wilaya ya Kaliua mkoani hapa kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa huo, Dk. Philemon Sengati.

Alisema kuwa udiwani ni kazi ya utumishi wa wananchi ila siyo ya ajira hivyo madiwani wanapaswa kuwa na miradi binafsi itakayowaongezea kipato nje ya posho za vikao na ile ya kila mwezi ili kujiweka vizuri kiuchumi.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora Msalika Robert Makungu (wa pili kutoka kushoto) akishiriki na Viongozi wenzake wa wilaya ya Kaliua kwenye ufunguzi wa kikao cha kwanza cha baraza la madiwani wa halmashauri ya wilaya hiyo juzi, Picha na Allan Vicent. 

Alibainisha kuwa pamoja na kuwatumikia wananchi wanapaswa kuhakikisha mambo yao ya kiuchumi yanakuwa vizuri ili baada ya kumaliza muda wao wa miaka mitano familia zao zisipate shida na hata wakitaka kugombea tena wasiaibike.

“Ndugu zangu udiwani sio ajira, anzisheni miradi ya kiuchumi itakayowaingizia kipato zaidi, ili mtakapomaliza muda wenu wa miaka mitano mambo yenu yawe mazuri,” alisema.

Makungu alisisitiza kuwa uchaguzi umeisha sasa ni wakati wa kuchapa kazi hivyo akawataka kutekeleza wajibu wao kwa kuzingatia kanuni, taratibu na sheria zilizowekwa.

Aidha, aliwataka kuwa kielelezo kizuri kwa wananchi wanaowaongoza na kuwa waadilifu na waaminifu katika utekelezaji wa majukumu yao ikiwemo kuhakikisha fedha na mali za halmashauri zinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa.

“Tunataka mabadiliko makubwa ya kiutenda katika halmashauri zetu, tunataka kuona mapato yakiongezeka na fedha zinazotolewa na serikali kwa ajili ya miradi ya maendeleo zitumike kwa kazi iliyokusudiwa na matokeo yaonekane,” alisema.

Msalika alibainisha kuwa Katiba ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Ibara ya 146 kifungu cha 2(c) inafafanua wajibu wa diwani kuwa ni kudumisha amani na utulivu na kuendeleza ustawi wa jamii katika eneo lake hivyo akawataka kutokuwa chanzo cha vurugu ndani ya vikao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles