23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

TCRA yapewa miezi mitatu vifurushi vya simu

Na Prisca Ulomi, WMTH

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dk. Faustine Ndugulile ametoa miezi mitatu kwa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kumaliza changamoto za bando na vifurushi
zinazotolewa na kampuni za simu za mkononi kwa wananchi.

Dk. Ndugulile ameyasema hayo leo Desemba 28, alipotembelea TCRA ikiwa ni moja ya taasisi zilizo chini ya Wizara hiyo kwa lengo la kufahamiana, kutambua majukumu yao na kuzungumza na Bodi, Menejimenti na wafanyakazi wa taasisi hiyo ili kuwa na uelewa wapamoja na kushirikiana kwa kufanya kazi kwa pamoja katika kuhudumia wananchi kuelekea Mapinduzi ya Nne ya Viwanda na kuiwezesha Tanzania kuwa na uchumi wa kidijitali.

Amesema, ni lazima TCRA ishughulikie malalamiko ya wananchi kwa kuwa wananchi hawana imani na vifurushi na bando, na kuwe na mfumo wa kuhakiki gharama halisi za mawasiliano kuendana na fedha aliyotoa mwananchi na kuwe na namba ya bure ambayo wananchi watapiga ili kuwasilisha malalamiko yao ili kuwawezesha wananchi kuongeza imani yao kwa serikali.

“Ni heri tufanye maamuzi mabaya kuliko kutokufanya maamuzi, nataka mshirikiane na Baraza la Watumiaji wa Huduma za Mawasiliano (TCRA – CCC) kumaliza changamoto hii kwa kuwa Watanzania sio wajinga, nataka aone kapata shilingi moja anaitumia shilingi moja yake kupiga simu,” amesema Dk. Ndugulile.

Pia, amewataka kuhakikisha kuwa, chaneli tano za bure za runinga inaonekana hata baada ya muda wa kulipia kumalizika kwa kuwa chaneli hizo hazionekani kwenye baadhi ya ving’amuzi.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Mhandisi Kundo Mathew ameipongeza TCRA kwa kutengeneza mifumo ya TEHAMA, kutambua changamoto zilizopo na imejipanga kuzifanyia kazi kwa kuwa lazima TEHAMA ichukue nafasi yake na itufikishe watanzania tunakotaka kwenda

Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Zainab Chaula amewataka wafanyakazi wa TCRA kujiongeza na kujituma zaidi badala ya kusubiri maagizo na maelekezo kwa kuwa wao ni wataalamu, hivyo washirikiane kwa pamoja ili kuhakikisha kuwa wanaendelea kuwahudumia watoa huduma na watumiaji wa huduma za mawasiliano.

Hata hivyo Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Mhandisi James Kilaba amekiri kuwepo wa changamoto za bando na vifurushi na ameahidi kuzifanyia kazi kwa kuwa TEHAMA imeongeza mnyororo wa thamani kwenye sekta zote na imesogeza huduma mbali mbali viganjani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles