24.8 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Pluijm aanza kazi Yanga ikiivaa Mbao

Hans van der PluijmNa ZAINAB IDDY-DAR ES SALAAM

KOCHA mkuu wa timu ya Yanga, Hans van der Pluijm, ameanza kazi rasmi ya kukinoa kikosi hicho kitakachoivaa Mbao FC leo katika Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Pluijm amerejea kikosini baada ya Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba kumshawishi kurejea kutokana na kocha huyo kujiuzulu kwake mwanzoni mwa wiki iliyopita.

Pluijm ameifundisha Yanga kwa zaidi ya misimu miwili sasa, alichukua maamuzi ya kubwaga manyanga kutokana na kile alichodai kudharauliwa kutokana na madai ya uongozi wa mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara, kumleta kocha George Lwandamina anayefundisha Zesco ya Zambia kuvaa viatu vyake pasipo kumpa taarifa.

Katika kuhakikisha kile alichokubaliana na waziri huyo, Pluijm jana alitinga mazoezini katika Uwanja wa Uhuru ilipokuwa ikifanya mazoezi Yanga na kuendelea na majukumu yake.

Kabla ya kuanza mazoezi, Pluijm aliwaita wachezaji na kuwaeleza kuwa amerejea kikosini hivyo anahitaji ushirikiano wa wachezaji na viongozi wenzake wa benchi la ufundi huku akiwataka pia kusahau yaliyotokea.

“Nimerudi kufanya kazi yangu, nahitaji ushirikiano wenu ili kuipa mafanikio Yanga, lakini pia naomba tuyasahau yaliyotokea na kufungua ukurasa mpya, ninamini niliishi vizuri na nyinyi wote, sitarajii kuona kunakuwa na jambo litakalonikwamisha kwenye utendaji wangu wa kazi,” alisema.

Wakizungumza na MTANZANIA Jumapili baadhi ya wachezaji wa Yanga juu ya kurejea kwa kocha huyo, walisema wamefurahi kuona amerejea kwani bado walikuwa wakihitaji mchango wake katika kufikia malengo waliyoyaweka kwa pamoja msimu huu wa ligi.

Nahodha wa kikosi hicho, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ alisema kuwa kama wachezaji hawatakiwi kuchagua mwalimu wa kuwafundisha kwani kilichowapeleka Yanga ni kucheza mpira, hivyo suala la kujiuzulu kwake ilikuwa pigo kwa kuwa ni ghafla lakini kurudi kwake pia kunaongeza uweledi kwako kwa kuona kocha wao bado anahitajika kufanya kazi nao.

Katika mechi hiyo na Mbao, iwapo kama Yanga itashinda itafikisha pointi 27.

Katika mwendelezo wa ligi hiyo, timu ya Ruvu Shooting itaikaribisha Stand United katika Uwanja wa Mabatini uliopo Mlandizi mkoani Pwani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles