24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Mpinzani wa Putin amepewa sumu?

MOSCOW, URUSI

KIONGOZI wa upinzani nchini Urusi, Alexei Navalny, amelazwa  huku madaktari wake wakichukua vipimo kubaini kile kilichosababisha kuugua ghafla wakati ripoti za awali zikionyesha amepata mzio mkali uliosababisha kuvimba uso, na kupata vipele vyekundu mwili mzima.

Navalny ambaye anatumikia kifungo cha siku 30 jela aliugua  ghafla akiwa gerezani Jumapili na alipelekwa hospitali siku hiyo hiyo asubuhi.

Anatumikia kifungo cha siku 30 kwa kuitisha maandamano ambayo hayakuwa na kibali ya kupinga kuachwa nje kwa wagombea wa kujitegemea katika uchaguzi wa Baraza la Jiji la Moscow.

Ripoti ya awali inaeleza kuwa Navalny  anasumbuliwa na mzio (allergy),  ambao umesababisha uso kututumka, kiasi cha kuathiri macho yake na kutokwa na vipele mwili mzima.

Hata hivyo daktari binafsi wa Navalny amesema mteja wake hajawahi kusumbuliwa na mzio hapo kabla, na kwamba labda amewekwa na mawakala  fulani wa sumu.

Timu yake ya madaktari walisema waliweza kuonana naye jana na waliandaa sampuli za nywele zake, na fulana aliyokuwa amevaa ili viweze kufanyiwa uchunguzi huru.

Wakati madaktari wake wakitaka uchunguzi huru wa afya yake, wale wanaomtibu jana walisema yuko katika hali ya kuridhisha. 

Msemaji wake, Kira Yarmysh amesema Navalny hakuwa na historia ya matatizo ya mzio na aliwasili katika hospitali akiwa na uvimbe mkali usoni na vipele vyekundu mwilini. 

Daktari wake wa kibinafsi Anastassia Vassilieva kisha alisema baadaye kwenye ukurasa wake wa Facebook baada ya kumtembelea hospitalini kuwa hawawezi kufuta uwezekano kuwa ngozi yake iliwekewa sumu na kuharibiwa na mtu mwingine

Navalny ni mpinzani maarufu nchini Urusi ambaye amekuwa akiilaza macho serikali ya Putin kutokana na ukosoaji wake wa maneno.

Ingawa hakuna uthibitisho wowote kama Navalny amelishwa au kuwekewa sumu lakini madaktari na wafuasi wake wana shauku ya kujua kilichosababisha hali hiyo iliyompata ghafla.

Miaka miwili iliyopita Navalny alishambuliwa katika jicho lake la kulia baada ya kuunguzwa na kemikali aliyomwagiwa na mtu mmoja.

Mtu huyo alimwagia usoni kemikali hiyo iliyokuwa na rangi ya kijani. 

Pamoja na hayo mchambuzi na siasa za Urusi, Steve Rosenberg anasema ni mapema mno kuhitimisha kwamba hali yake ya kiafya ya sasa  ina uhusiano na mtazamo wake wa kisiasa au harakati zake.

Taarifa za kwenye vyombo vya habari zinasema kuwa karibu watu 20,wakiwamo waandishi wa habari walikamatwa juzi  baada ya kukusanyika nje ya hospitali ambayo Navalny anatibiwa.

Jana vyombo vya habari vya Urusi viliripoti kuwa waandamanaji wengi waliokamatwa  mwishoni mwa wiki wameachiwa.

Ingawa karibu watu 150 waliokamatwa  pamoja na Navalny walikuwa bado wako ndani jana  wakisubiri kufikishwa mahakamani kushitakiwa kwa kufanya maandamano yasiyokuwa na kibali.

Navalny mwenye umri wa miaka 43, alitarajiwa kushindana na Rais Vladmir Putin katika uchaguzi wa mwaka jana lakini alizuiwa kwa sababu ya hukumu ya mashitaka ya ulaghai ambayo yeye na wafuasi wake wanasema ilichochewa kisiasa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles