24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Lumbesa, mifuko ya plastiki yadhibitiwa

mifukoNa UPENDO MOSHA, MOSHI

BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya Manispaa ya Moshi mkoani Kilimanjaro, limepitisha sheria mbili za kudhibiti utumiaji wa mifuko ya plastiki pamoja na kudhibiti ufungaji wa mazao kwa mtindo wa lumbesa.

Akizungumza katika kikao cha baraza la madiwani kilichofanyika jana mjini Moshi wakati wa mjadala wa kupitisha sheria hizo, Meya wa Manispaa hiyo, Raymondy Mboya, alisema sheria  ya kudhibiti matumizi ya mifuko ya plastiki ina lengo la kulinda mazingira na afya za Wananchi, wakati sheria ya lumbesa inalenga kuwasaidia wakulima kiuchumi.

“Halmashauri yetu tumepiga hatua kubwa  kwa kupitisha sheria hii ya kudhibiti matumizi ya mifuko ya plastiki ambayo ina lengo kubwa la kutunza mazingira na afya za wananchi wetu pamoja na sheria ya ufungaji wa mazao kwa mtindo wa lumbesa.

“Sheria hii ya Lumbesa itawasaidia wakulima kuuza mazao yao vizuri na kupata faida, tofauti na ilivyo sasa ambapo wafanyabiashara wamekuwa wakiwanyonya wakulima kwa njia hiyo.

“Hiyo Sheria ya Lumbesa imepitishwa bila kipingamizi na wajumbe wote wa baraza, wakati sheria ya matumizi ya mifuko ya plasiti imepitishwa kwa kupigiwa kura na madiwani 28 wakiwamo 16 walioikubali na 10 walioikataa.

“Matumizi ya mifuko ya plasitii ni hatari kwa afya za wananchi kwani kwa mujibu wa taarifa za wataalamu wa afya, mifuko hiyo imekuwa ikisababisha magonjwa mbalimbali ikiwamo kansa na ugumba.

“Kwa hiyo, huu ni wakati wa wananchi kujiandaa kuachana na matumizi ya mifuko hiyo kwa sababu sasa sheria ya kuizuia imepitishwa,” alisema Mboya.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa hiyo, Michael Mwandezi, alisema sheria hizo zitaanza kutumika baada ya mamlaka husika kuzisaini.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles