31.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Lowassa ataka wenye uhitaji wasaidiwe

Pg 2Na Jonas Mushi, Dar es Salaam

WAZIRI Mkuu wa zamani na aliyekuwa mgombea urais wa Chadema kwa mwamvuli wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Edward Lowassa, ametoa wito kwa jamii kuwasaidia watu wenye uhitaji.

Alitoa wito huo jana baada ya kutembelea vituo vitatu vya watoto yatima   jijini Dar es Salaam na kutoa vyakula kwa ajili ya futari katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Vituo alivyovitembelea ni   Makao ya Kulea Watoto Yatima na Wasio na Makazi Maalumu (CHAKUWAMA) cha Sinza Wilaya ya Kinondoni, Kituo cha Watoto Yatima cha UMRA  Magomeni na Kituo cha Watoto Yatima cha Khayrat  Kigogo.

Alitoa pia pongezi kwa waanzilishi wa vituo hivyo na kuwatia moyo  kuendelea kusaidia watoto wanaoishi katika mazingira magumu kwa vile  kufanya hivyo ni kuisaidia jamii nzima.

Akiwa katika Kituo cha CHAKUWAMA, Lowassa alisema ataendelea kutoa ushirikiano katika kusaidia watoto wenye mahitaji huku akiwaasa wazingatie elimu na mafunzo ya dini zao.

“Tutaendelea kuwaunga mkono katika kuwalea watoto hawa na nitoe wito kwa jamii kuwasaidia watu wenye mahitaji kama watoto yatima ili tushirikiane kwa pamoja kuwalea kwa sababu ndiyo jamii yetu,” alisema Lowassa.

Akitoa shukrani kwa msaada huo, Mwanzilishi wa Kituo hicho, Saida Hassan, alisema kituo  kilianza na watoto watano lakini sasa kina watoto 90 hivyo kufanya uhitaji kuwa mkubwa zaidi.

“Tunaomba viongozi wetu wafuate nyayo za Lowassa kuwakumbuka na kuwasaidia watu wenye uhitaji kama watoto hawa ambao wamezidi kuongezeka kadiri siku zinavyokwenda,”  alisema Saida.

Akiwa katika kituo cha UMRA,   Mlezi wake   Rahma Kishumba, alisema  aliipokea ziara ya Lowassa kwa furaha na kwamba ana amini kufika kwake kutakua chachu kwa viongozi wengine kuguswa na kuwasaidia watu wenye uhitaji.

Alisema kituo chake kina watoto 90, wasichana 44 na wavulana 46 na   changamoto kubwa ni gharama za elimu kwa watoto hao.

“Nimepokea ziara ya  Lowassa kwa furaha kubwa naomba  aendelee na moyo huu kwa sababu  Mungu ataendelea kumbariki,” alisema Rahma.

Kwenye kituo cha Khayrat, Lowassa alitoa pongezi kwa waanzilishi  wa vituo vya watoto yatima na kuwataka waendelee na moyo huo na  ataendelea kuwatembelea mara kwa mara.

“Napenda kuwapongeza sana kwa hatua mlizochukua za kuwasaidia watoto wanaoishi katika mazingira magumu si kwa sababu mna uwezo bali kwa sababu mna moyo wa kusaidia,” alisema Lowassa na kuongeza:

“Nimeona niwatembelee na niwaletee watoto chakula kidogo kwa ajili ya futari, nawatakieni Ramadhani njema na Mungu apokee funga zenu.”

Mlezi wa Kituo cha Khayrat, Hadija Hussein alisema wanategemea sana misaada ya watu kwa sababu watoto hao hawana ndugu wala wazazi wa kuwasaidia.

“Hapa tuna watoto 64 ambao wanahitaji chakula, mavazi na elimu na wengine ni wadogo wanaohitaji uangalizi mkubwa kutoka kwa walezi,” alisema.

Akiwa katika kituo cha Khayrat, Lowassa aliombewa dua na watoto wawili ili Mungu amtunze siku zote za maisha yake na endelee na moyo wake mwema.

Katika hatua nyingine, Lowassa aliendelea kulaani serikali kutowasikiliza wapinzani na kwamba chama chao kinaendelea kulishughulikia suala la kukatazwa kufanya mikutano na makongamano ya  siasa.

“Nasikitika sana serikali kukosa uvumilivu wa kuvisikiliza vyama vya upinzani lakini Mwenyekiti wangu, Freeman Mbowe anashirikiana na viongozi wengine kuhakikisha suala la kuzuiliwa mikutano ya hadhara linapata ufumbuzi,” alisema Lowassa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles