Na Mwandishi Wetu
TIMU ya Manispaa ya Kinondoni, KMC mambo yameendelea kuwa magumu baada ya kukosa ushindi katika mchezo wa tano mfululizo kwa kufungwa na Kagera Suga bao 1-0 kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
Katika mchezo huo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, uliopigwa leo Oktoba 29,2021, bao pekee la Kagera Sugar limefungwa na Meshack Abraham dakika ya 17.
Baada ya mchezo huo, wachezaji wa KMC walionekana wakisononeka baadhi yao akiwamo kipa Farouk Shikalilo wakikaa chini na kuzunika.
Kocha Msaidizi wa KMC, Ahmady Ally, amezungumzia mchezo huo na kusema wamepoteza kutokana na kukosa umakini na wapinzani wao kutumia nafasi hiyo na kukiri kuwa wanahitaji kuongeza nguvu.
“Hatuko vizuri kwa kweli, tunatakiwa kujiangalia na muda huu wa mapunziko inatakiwa kujipanga kujirekebisha kwa sababu ligi ni ngumu,” amesema Ally.
Mchezo mwingine wa leo uliikutanisha Mbeya Kwanza na Biashara United ambao walitoka sare ya bao 1-1 kwenye Uwanja wa Sokoine, Mbeya.