Na Winfrida Mtoi, Mtanzania Digital
JUMLA ya mapambano 14 yanatarajia kupigwa kesho Oktoba 30, 2021 katika usiku wa ‘Dar Boxing Derby’ ambapo leo Oktoba 29,2021 mabondia wamejitokeza kupima uzito wakishuhudiwa na mashabiki waliofurika kwenye Uwanja wa Kinesi, Dar es Salaam.
Mapambano makubwa yatamkutanisha Francis Miyeyusho dhidi ya Adam Kipenga na Iddi Piarali atatwangana na Ramadhan Shauri.
Aidha Selemani Kidunda atachapana na Jacob Maganga kupigania ubingwa wa Taifa wa Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBRC) uzito wa ‘super middle’.
Pambano mengine yenye ushindani ni kati ya Grace Mwakamele na Asha Ngedele, Ismail Galiatano dhidi ya Allan Kamote, George Bonabucha atapigana na Haji Juma.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Miyeyusho amesema ataendeleza ubabe wa kuwapiga mabondia wote wa Mabibo na Manzese, huku Kibenga akitamba kuzima ngebe za mpinzani wake huyo.
“Ninachoomba tu kesho Adam Kipenga awahi uwanjani nimuoneshe kwa sababu leo siku ya kupima uzito tu kakimbia amechelwa, asije akakimbia,” ametamba Miyeyusho.
“Mimi nimechelewa kwa sababu nilikuwa nafanyia mazoezi Afrika Kusini nimetua leo saa tano na ndenge, foleni ikanichelewesha, siogopi wala nini nampiga mapema tu Miyeyusho. Tumechoka dharau watu wa Mabibo,” amesema Kipenga.
Naye Kidunda ameahidi kupeleka mkanda jeshini, kwani atahakikisha anampiga Maganga kwa TKO.
“Mimi ni mtu mbaya wote wananijua, nimejiandaa vizuri, nitampiga vibaya Jacob Maganga,siongei sana watu waje Kinesi kuona ngumi,” ametamba Kidunda.
Kwa upande wake Promota wa mchezo huo, Kapteni Selemani Semunyu, amewataka mashabiki kufika mapema kwa sababu wataweka pia TV kubwa ili wale mashabiki wa soka kushuhudia mechi ya Yanga na Azam.
“Mapambano yataanza mapema, saa 12:00 jioni, ulinzi upo wa kutosha, pia mashabiki wa soka tutawafungia screen kubwa kuangalia mechi ya kesho, huku wakishudia ndondi,” amesema Kapteni Semunyu.