ZAIDI ya kaya 200 katika Kijiji cha Ipota, wilayani Mlele, mkoani Katavi, hazina mahali pa kuishi baada ya nyumba zao kuteketezwa kwa moto na askari wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa madai si makazi rasmi.
Tukio hilo lilizua taharuki kubwa kwa wakazi wa kijiji hicho ambao kwa siku mbili sasa familia zote zinalala nje.
Katika familia hizo wapo watoto wadogo, wajawazito na wazee ambao wameamua kuishi chini ya miti huku wakinyeshewa na mvua.
Inadaiwa askari wa Tanapa na polisi kutoka Kituo cha Polisi Kibaoni, waliteketeza nyumba za wakazi hao kwa moto juzi.
Kaimu Mwenyekiti wa Kijiji cha Ipota, Soguta Maduhu, akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea eneo hilo jana, alisema kaya 210 hazina makazi na msaada wa haraka unahitajika.
“Kaya 210 hazina makazi ya kuishi baada ya nyumba zao kuchomwa moto na askari wa Tanapa na polisi wamesababisha wananchi hawa kuishi kwa shida mno, licha ya mvua zinazoendelea kunyesha,” alisema Maduhu.
Akisimulia tukio hilo, Maduhu alisema askari hao walifika kijijini hapo kwa kushtukiza na kuteketeza kwa siku mbili mfululizo.
“Kaya hizi zimepata mateso makubwa, licha ya kuchomewa nyumba zao bado askari waliwapiga wananchi…hawakuwa na huruma kabisa, waliwapiga watoto, wajawazito na wagonjwa,” alisema.
Alisema kumekuwapo na mgogoro wa mipaka ya makazi kati ya Tanapa na wakazi wa kijiji hicho, Hifadhi ya Taifa ya Katavi, eneo tengefu la kijiji na uhifadhi wa misitu kwa muda mrefu sasa. Alisema nyumba hizo zinadaiwa kujengwa ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Katavi.
“Ukweli ni kwamba nyumba hizi zilijengwa mita 800 kutoka Hifadhi ya Taifa ya Katavi, utaratibu na sheria zilizopo wananchi wanatakiwa kujenga makazi yao umbali wa mita 500 nje ya hifadhi,” alisema Maduhu.
Kutokana na hali hiyo, aliuomba uongozi wa Serikali ya Mkoa wa Katavi kufika kijijini hapo kupima mipaka ili ukweli ujulikane.
Kwa upande wake, Joseph Kalubwa alisema mipaka inayotenganisha hifadhi hiyo na kijiji hicho ni ya asili.
Naye mkazi wa kijiji hicho, Samwel Kisinja, alidai familia yake yenye watu wapatao 32 tangu juzi wamelazimika kulala chini ya miti usiku kucha, baada ya makazi yao kuteketezwa kwa moto na askari hao.
Mkazi mwingine, Maria Mchelu, alisema mbali ya kuchomewa na nyumba yake, askari waliteketeza magunia yake matatu ya chakula.
Naye Deus Kuhanda alisema wakazi hao wameishi eneo hilo zaidi ya miaka 20.
Mbunge wa Mlele, Dk. Pudensiano Kikwembe, alikiri kupokea taarifa hizo na kuahidi kuwasiliana na uongozi wa mkoa mara moja.