KITUO cha Redio Efm kimetenga jumla ya Sh milioni 3 kwa washindi wa mchezo wa Sakasaka 2016 unaofanyika kwa mwaka wa pili baada ya kupata mafanikio mwaka jana.
Mkuu wa Kitengo cha Matukio na Mawasiliano, Neema Mukurasi, alisema shindano hilo huchezeshwa kwa kuficha kitu katika eneo mojawapo kisha msikilizaji wa redio hiyo hutakiwa kusikiliza maelekezo kisha kwenda kutafuta kitu hicho kilichofichwa ndipo hujishindia zawadi hizo.
Alisema mchezo huo kwa mwaka huu unatarajiwa kuanza Juni 12 kwa wilaya tano, Kinondoni, Ilala, Temeke, Mkuranga na Kisarawe.
“Idadi kubwa ya wasikilizaji wetu wana changamoto nyingi za maisha hivyo sisi Efm tunawawezesha kupitia vitu tofauti tofauti ambavyo vitawasaidia kujikwamua kimaisha,” alisema.