31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Demba Ba avunjika mguu

Demba Ba
Demba Ba

SHANGHAI, CHINA

NYOTA wa zamani wa klabu ya Chelsea na Newcastle, Demba Ba, amevunjika mguu juzi katika mchezo wa ligi kuu nchini China.

Mchezaji huyo amevunjika vibaya wakati anawania mpira dhidi ya mpinzani wake nahodha wa Shanghai SIPG, Sun Xiang.

Tukio hilo lilitokea katika dakika ya 64 ya mchezo huo timu ya Demba Ba, Shanghai Shenhua, ilipokutana na watani wao wa jadi, Shanghai SIPG, ambapo mchezo huo ulimalizika kwa kikosi cha Demba Ba kushinda mabao 2-1.

Demba Ba mwenye umri wa miaka 31, inadaiwa ameumia vibaya tofauti na wachezaji wengine ambao walivunjika kwa kipindi cha miaka ya hivi karibuni kama ilivyo kwa Eduardo Silver wakati yupo klabu ya Arsenal mwaka 2008, alipovunjwa na Martin Taylor au Ryan Shawcross alipomvunja mguu Aaron Ramsey, wakati wa kuwania mpira.

Uongozi wa klabu hiyo ya nchini China, umesikitika kuona mchezaji wao atakuwa nje ya uwanja kwa kipindi kirefu huku akiwa ni mfungaji bora katika ligi hiyo ambapo hadi sasa ana jumla ya mabao 14 kati ya michezo 18 aliyocheza.

Kocha mkuu wa timu hiyo, Gregorio Manzano, amedai kwamba wapo katika masikitiko makubwa kwa kuwa wanaamini watamkosa mchezaji huyo mwenye uwezo mkubwa wa kupachika mabao.

“Kikosi kwa sasa kitakuwa na wakati mgumu hasa katika safu ya ushambuliaji baada ya Demba Ba kuvunjika mguu, ni jambo la kusikitisha sana kwa klabu kumkosa mchezaji huyo.

“Ninaamini atarudi uwanjani lakini itachukua muda mrefu, hivyo timu yetu inaweza kuyumba kutokana na kumkosa mchezaji huyo japokuwa kuna wachezaji wengine ambao wanaweza kuziba nafasi hiyo.

“Ni tatizo ambalo linaweza kumkuta mchezaji yeyote akiwa uwanjani, hivyo tunatoa pole kwake na tutaendelea kuwa pamoja na yeye kwenye kipindi hiki kigumu cha kuuguza mguu wake,” alisema Manzano.

Hata hivyo, kocha huyo anaamini kuwa kuvunjika huko mguu kwa mchezaji huyo, kunaweza kumsababisha akastaafu soka lake lakini inategemea atakuja kuwa katika hali gani.

“Demba Ba ameumia vibaya sana, kuna uwezekano mkubwa wa kuja kustaafu soka mara baada ya kupona, lakini inategemea atakuja kuwa katika hali gani baada ya kupona,” aliongeza.

Mchezaji huyo baada ya kuondoka Chelsea mwaka 2014, alijiunga na klabu ya Besiktas ya nchini Uturuki na kucheza michezo 29 huku akifunga mabao 18. Mwaka jana mchezaji huyo alijiunga na klabu hiyo ya nchini China kwa uhamisho wa kitita cha pauni milioni 12.

Tangu amejiunga na klabu hiyo ya nchini China, amefanikiwa kucheza jumla ya michezo 29 ya ligi kuu na kufanikiwa kushinda mabao 20.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles