23.3 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

DC Ileje apiga marufuku wazazi kwenda na watoto vilabuni

*Wazazi watakaobainika kufanya hivyo kukamatwa

*Aagiza wanafunzi kupata chakula cha mchana shuleni

Na Denis Sikonde, Songwe

Wakati Mkoa wa Songwe ukiwa katika ajenda endelevu ya kupambana na udumavu imeelezwa kuwa wilayani Ileje wazazi wamekuwa chanzo cha kukwamisha jitihada hizo kwa kuwanywesha pombe za kienyeji watoto wadogo na kushinda nao vilabuni bila kuzingatia afya ya mtoto .

Wananchi wakimsikiliza Mkuu wa Wilaya ya Ileje, Anna Gidarya.

Agizo hilo limetolewa Mei 7, mwaka huu na Mkuu wa Wilaya ya Ileje, Anna Gidarya wakati akipokea na kutatua changamoto zinazowakabili wananchi katika vijiji mbalimbali wilayani humo.

Gidarya amesema baadhi ya wanawake wilayani humo wamekuwa na tabia ya kuwanywesha watoto wadogo pombe za kienyeji kwenye vilabu vya pombe za kienyeji hali ambayo husababisha kuendelea kwa udumavu kwa watoto wadogo.

Gidarya amesema kuanzia sasa ni jukumu la watendaji wa kata zote 18 zinazounda wilaya hiyo kuhakikisha wanafanya misako kwenye vilabu vyote vya pombe za kienyeji kuwakamata wanawake wote ili kurekebisha tabia za wazazi kurithisha watoto tabia mbovu.

“Naagiza wanawake wote watakaokutwa na watoto wadogo kwenye vilabu vya pombe za kienyeji wakamatwe ili kuhakikisha ajenda ya lishe inakuwa ni ya kila mwananchi ili kuondoa tatizo la udumavu kwa wilaya yetu ya Ileje na mkoa wa Songwe kwa ujumla.

“Sambamba na hilo kuanzia Julai, 2022 kwa shule zote za msingi na sekondari viongozi wa kijiji kwa kushirikiana na kamati za shule hakikisheni wanafunzi wanakula chakula cha mchana shuleni ili kusaidia kuongeza kiwango cha ufaulu pamoja na kuondoa udumavu,” amesema Gidarya.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Ileje, Pastori Mashiku amesema kila Mtendaji wa kijiji na kata kwa kushirikiana na kamati za afya kuendelea kutoa elimu ya lishe kupitia mikutano ya hadhara ili kila mwananchi achukulie uzito lengo likiwa ni kutokomeza tatizo la udumavu wilayani humo.

Upande wake, Ester Kamendu mkazi wa kijiji cha Mbebe alisema akina mama wameona ni kawaida kwenda vilabuni na watoto wadogo, hivyo agizo la kuwakamata litakuwa limenusuru afya za watoto kwani hunyweshwa pombe wakiwa na umri mdogo.

Marko Mbwagha mkazi wa kijiji cha Ikumbilo ambaye alisema kupuuzwa kwa elimu ya lishe kunasababisha baadhi ya wanawake kuwanywesha pombe watoto wao hivyo watakaokamatwa itakuwa mfano kwa wengine.

“Mkakatiu huu utakuwa ni ajenda kwenye mikutano ya hadhara kupitia wataalamu wa afya na lishe ngazi za kata na vijiji,” amesema Mbwagha.

Mkoa wa Songwe unashika nafasi ya tatu kitaifa katika uzalishaji wa mazao ya chakula lakini hali ya udumavu kwa watoto chini ya miaka 5 ni asilimia 43.3 jambo linalosababishwa na wananchi kukosa elimu ya chakula bora.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles