21.5 C
Dar es Salaam
Saturday, July 27, 2024

Contact us: [email protected]

DC Ileje akabidhi mkopo wa pikipiki 10 na bajaji 2 kwa vijana

Na Denis Sinkonde, Songwe

Mkuu wa Wilaya ya Ileje mkoani Songwe, Anna Gidarya amekabidhi pikipiki 10 na bajaji mbili ikiwa ni sehehemu ya fedha inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa vikundi viwili vya bodaboda wilayani humo sambamba na mfano wa hundi ya Sh milioni 100.2 ikiwa ni sehemu ya mkopo wa vikundi vya vijana, wanawake na walemavu.

Mkuu wa Wilaya ya Ileje, Anna Gidarya akikabidhi pikipiki 

Hafla ya kukabidhi pikipiki, bajaji na hundi imefanyika Machi 18, 2022, katika stendi ya basi Itumba wilayani humo wakati wa kuadhimisha siku 365 za kukaa madarakani Rais wa Awamu ya Sita, Samia Suluhu Hassan.

Gidarya amesema Serikali imetoa mikopo hiyo ya bajaji na pikipiki kwa lengo la kuwasaidia kuwainua kiuchumi na si kugeuza kuwa vikwazo kwa familia zao kama fimbo ya kuwanyanyasa wananchi bali wawe mabalozi wema wa kuhamasisha vijana kukopa na kueleza faida za mikopo.

“Wakati mnatumia vyombo hivi endesheni kwa kufuata sheria za usalama barabarani na kujiepusha na ubebaji wa magendo kwa kutumia vyombo hivi kutokana na wilaya ya Ileje kupakana na nchi jirani za Malawi na Zambia.

“Mkuu wa polisi wilaya hakikisha unatoa elimu kwa vijana hawa ili kuwakumbusha sheria za usalama barabarani namna wanavyopaswa kushirikiana na jeshi la polisi kufichua vitendo vya kiuharifu pindi wanapoyabaini wakati wakitekeleza majukumu yao,” amesema Gidarya.

Gidarya amesema mikopo ya asilimia 10 bila riba ni takwa la kisheria kwa kila halmashauri nchini kutenga kwa ajili ya kuviwezesha vikundi vya wanawake kukopa 4%, vijana 4% na watu wenye ulemavu 2%, hivyo amewasihi wanavikundi walionufaika na mikopo hiyo kurejesha kidogo kidogo ili vikundi vingine vikope kwa ajili ya kujikwamua kiuchumi.

Gidarya ametumia nafasi hiyo kuipongeza serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu kwa kutoa fedha za miradi ya maendeleo kwa upande wa afya, elimu, maji, barabara na TANESCO kwa ajili ya kuondoa adha kwa wananchi.

“Mpaka sasa serikali imetoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa jengo la wagonjwa mahututi ICU Sh milioni 250 katika hospitali ya wilaya ya Ileje ambapo ujenzi umeanza, ujenzi wa shule ya wasichana kata ya Chitete Sh milioni 470, ujenzi nyumba za watumishi katika kituo cha afya Lubanda milioni 90,  ujenzi shule ya msingi Kitongoji cha Ipapa Kijiji cha Isongole kwa gharama ya Sh milioni 400 pamoja na ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kutoka Vwawa -Izyira-Mlale Ileje mpaka makao makuu ya wilaya Itumba,” alisema Gidarya.

Upande wake Afisa Maendeleo ya Jamii wilayani Ileje, Rodrick Sengela amesema kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2021/2022 halmashauri hiyo ilitenga kiasi cha fedha zaidi ya Sh milioni 84 kwa ajili ya vikundi vya wanawake, vijana na walemavu ambapo mpaka sasa halmashauri imetoa mkopo wa zaidi ya Sh milioni 90.

Mwenyekiti wa halmashauri ya Ileje, Ubatizo Songa amesema katika siku 365 za kukaa madarakani Rais Samia wamefanikiwa kuongeza ukusanyaji wa mapato kutokana na ushirikiano baina ya watalamu kutoka ofisi ya mkurugenzi, ofisi ya mkuu wa wilaya na ofisi ya Chama Cha Mapinduzi(CCM) wilaya pamoja na wananchi na kuifanya Ileje kushika nafasi ya tatu kimkoa kati ya halmashauri tano za mkoa wa Songwe, nakwamba ameiweze kutoa mikopo kwa vikundi kutokana na mapato ya ndani.

Akitoa shukurani kwaniaba ya vijana hao, Amosi Mwanja ameupongeza uongozi wa Jumuiya ya Vijana (UVCCM) Ileje ikiongozwa na Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo maoni Mbuba kwa kuhamasisha vijana kukopa kwa kuunda vikundi, hivyo kuahidi kutumia mkopo huo kujikwamua kiuchumi na kurejesha kwa wakati ili wengine wanufaike.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles